Search This Blog

Monday, October 24, 2022

TIMBWILI...TIMBWILI - 2

 





    Chombezo : Timbwili .... Timbwili

    Sehemu Ya Pili (2)





    BAADHI ya wanywaji na walaji walimwona, na walimtazama kwa makini, sekunde chache kwake na sekunde chache kwa Halima. Watu hao walimjua vizuri Saad, kuwa ni mtoto wa town. Na pia walimjua vizuri Halima, kuwa ni mkewe Saad. Lakini waliishia kuwatazama tu, hakukuwa na yeyote aliyeweza kubashiri ni kipi ambacho kingetokea.



    Hawakuwa hao wanywaji na walaji pekee waliomwona. La. Hata Halima alimwona. Hata Nsanzugwanko alimwona!



    Kila ambaye Saad alimtupia macho alikuta naye akimwangalia. Akasonya kwa hasira. Ni heri nisingekuja, alijisemea kwa mnong'ono ambao hakuyafikia hata masikio yake mwenyewe.

    Pia, akawaza kuwa, ingekuwa vyema kama asingeyajali maneno aliyoambiwa na Mwajuma; angeenda zake nyumbani ambako asingeigundua siri hii iliyofichuka kiasi cha kuunyong'onyesha moyo wake kwa kiwango kisichokadirika.



    Lakini alikuwa amechelewa. Na macho ya waliomtazama ni kama vile yalikuwa yakimwambia, “Saad we’ ni mwanamume. Usikubali huyo mwanamke akuvunjie heshima. Mshughulikie yeye na mjinga-mjinga wake.”



    Angeweza?



    Ukweli ni kwamba, hasira zilishamtawala. Alitamani kumfuata Halima pale na kumfunza adabu. Amzabe makofi matatu yenye uzito wote nyuma yake. Na iwe ni palepale ukumbini!

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hata hivyo papohapo wazo jingine lilimjia akilini. Kwamba, afikiri kwanza na kuyatafakari matokeo ya hatua yoyote aliyotarajia kuichukua wakati huo. Ni hilo lililomtisha.



    Nsanzugwanko alijaaliwa umbo kubwa na alikuwa ni mkorofi. Hapo DDC Kariakoo walikuwa na rekodi yake ya kuwashushia vipigo vya 'mbwa mwizi' wanaume wawili waliompapasa makalio mwanamke mmoja aliyekubaliana naye kustarehe pamoja siku hiyo. Wakware hao walimfanyia vitendo hivyo mwanamke huyo wakati alipoanza kucheza muziki uliopigwa na bendi fulani maarufu jukwaani.



    Alicheza kwa kunengua kiuno kwa umahiri mkubwa na ndipo wakware hao walipomfuata na kuanza kumpapasa. Kilichofuata hakikutofautiana na gharika kwa wale wakware.



    Siku hiyo Saad aliishuhudia songombingo hiyo, na alikiri kuwa Nsanzugwanko ana ubavu wa kupambana na zaidi ya mwanamume mmoja. Ni hilo lililomfanya jioni hii asitishe kufanya chochote kile kitakachomkera Nsanzugwanko. Hakuwa na ulemavu wowote maungoni mwake, na alihitaji kuendelea kuwa hivyo.



    Lakini, je, asipowavaa Nsanzugwanko na Halima hapo walipo, wateja wengine watamchukuliaje? Hawatamchukulia kama 'mume bwege'?



    Akawakazia macho Halima na Nsanzugwanko. Macho yake na ya Halima yakakutana. Aliyaona macho ya Halima kama vile yanayomwambia, 'Acha paniki. Jihadhari. Ukizua sheshe la aina yoyote utakuja juta baadaye.'



    Akanywea na kubaki akiwatazama kwa uchungu. Hatimaye akatupa macho kulia kwake ambako aliona viti viwili vilivyokuwa tupu huku cha tatu kikiwa na mteja, mwanamume aliyeonesha bayana kukolewa na kilevi.



    Hakumsalimia mtu huyo, alivuta kiti na kuketi. Mhudumu alipomjia alimwagiza soda baridi. Dakika chache baadaye alikuwa akinywa soda hiyo huku macho yakiwa hayabanduki kwa mkewe, Halima na Nsanzugwanko walioonekana wakinywa bia zao kimyakimya.



    Muda mfupi baadaye walinong'onezana kisha wakasimama.

    Wakaondoka kwa mwendo wa asteaste. Wakapita jirani na meza iliyopakana na ile aliyokuwepo Saad. Yule mtu aliyekolewa na kilevi aliwatazama kisha akamtazama kidogo Saad na kusonya.

    Saad hakuujali msonyo wa mtu huyo na labda pia asingemjali kama, pamoja na kulewa kwake asingesema, “Wanawake! Wanawake s'o watu. Huyo mwanamke nasikia ni mke wa mtu, lakini hajatulia. Kama mimi nd'o ningekuwa mumewe, na nikagundua....” akaiacha sentensi hiyo ikielea.



    Yalikuwa ni maneno yaliyopenya masikioni mwa Saad mithili ya ngurumo ya radi na kutua moyoni kama kaa la moto. Yalimuuma!

    Bila hata ya kuimaliza soda yake alinyanyuka na kutoka. Alipofika nje hakuwaona wapenzi wale wawili; Halima na Nsanzugwanko!



    ***************



    “MAGOMENI, nyuma ya kanisa la Anglikana,” Nsanzugwanko alimwambia dereva teksi aliyewawahi mara tu walipotoka ukumbini.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Nusu saa baadaye walikuwa ndani ya 'gesti bubu' nyuma ya kanisa la Kianglikana, Magomeni ambako walizitumia pumzi zao katika kuikonga mioyo yao, Halima akifurahia kufanya kila ambalo Nsanzugwanko alipendekeza.



    Ni pale walipohisi uchovu miilini mwao, ndipo Nsanzugwanko alipomuuliza, “Vipi, utakwenda kwa bwana'ako au nd'o hadi kunakucha?”



    “Wewe tu,” Halima alijibu kwa sauti dhaifu, sauti ya mikogo-mikogo, mkono wake mmoja ukiwa mahala fulani mwilini mwa Nsanzugwanko ukipapasa kwa namna isisimuayo.



    Ilimlazimu Nsanzugwanko kumzuia na kusema, “Una vituko

    vinavyokwenda sambamba na jinsi ulivyoumbika. Unastahili kupewa tuzo...” akasita kidogo. Kisha akaongeza, “Jamaa yako katuona. Unadhani nyumbani patatosha?”



    Halima alisonya. “Achana nae bwege yule,” hatimaye alisema. “Hanibabaishi. Najua nitakavyoyamaliza.”



    Ilitosha. Wakaendelea na kuendelea, kila mmoja akitaka kuonekana ni zaidi ya mwenzie.



    Saa tatu usiku ikagota.



    Saa nne!



    Tano!



    Sita!



    Hatimaye jogoo akawika, Halima na Nsanzugwanko wakiwa mlemle chumbani, katika gesti ileile na wakiendelea kuyafanya yaleyale waliyoanza kuyafanya tangu walipoingia.



    ***************



    “TEKSI mjomba,” dereva mmoja alimwambia Saad baada ya kumwona akiangaza macho huku na kule, nje ya ukumbi wa DDC Kariakoo.



    Saad alimfuata. Dakika chache baadaye walikuwa barabarani, Saad akielekea nyumbani, Kigogo. Alifika na kufungua mlango, uchungu ukiwa unazidi kumtawala moyoni.



    Chumba hicho kikubwa kilikuwa kimya. Zaidi ya kelele za wanandoa wa chumba cha pili, kelele zilizopenya hadi chumbani humo, hakukuwa na sauti nyingine iliyoyafikia masikio yake.



    Akiwa na mikunjo ya hasira usoni pake, Saad aliangaza macho huku na kule chumbani humo na kupata picha halisi; Halima hajakanyaga hapo! Akapiga ngumi kiganjani na kufuatisha msonyo mkali. Akaanza kutembea huku na kule chumbani humo kama atafutaye kitu fulani.



    Mara akasitisha zoezi hilo, na kama vile aogopaye, alitupa macho kitandani. Akaitazama mito miwili ambayo ni kama vile ilikuwa ikimdhihaki. Akautazama mto mmoja kwa makini, mto ambao aghalabu Halima hukiegemeza kichwa chake kila usiku. Akauona unywele mrefu ambao ulisahaulika wakati Halima akitandika asubuhi.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Akaushika unywele huo na kuunusa. Mwili ukamsisimka kwa wivu, msisimko ambao hata hivyo ulitoweka haraka kama ulivyomjia.

    Akasonya na kuifuata kabati. Akafungua saraka moja na kutia kijitabu kidogo cha hadithi. Akaketi sofani na kujaribu kusoma.



    Hakikusomeka!



    Akahisi sauti ikimwambia, ‘unaweza kusoma kitabu au gazeti kwa amani huku ukijua kuwa muda huo mkeo yuko na mwanamume mwingine, na labda wakifanya yale unayofanya naye au hata zaidi ya hayo?’



    Akakiweka kando kitabu hicho. Papohapo akasimama na kuanza kukusanya vitu vyote alivyojua kuwa ni vya mkewe, Halima, akaviweka sofani. Miongoni mwa vitu hivyo, na ambavyo vilimshangaza na kumzidishia sononeko moyoni ni kondomu na vidonge vya uzazi wa mpango. Vitu hivyo vilikuwa ndani ya mkoba wa Halima.



    “Yaani...yaani kweli....” alinong'ona kwa kigugumizi huku akizitazama kondomu zile kama asiyeamini macho yake.



    Zikamjia kumbukumbu za maisha yake na Halima. Walishatimiza miaka miwili tangu walipofunga ndoa, na walijaaliwa kupata mtoto mmoja. Lakini kwa Halima huyo alikuwa ni mtoto wa pili; mtoto wa kwanza alimzaa wakati akiwa na mwanamume mwingine.



    Kwamba Halima alikwishafanya mapenzi na wanaume wengine kabla hawajafunga ndoa, hilo halikuwa ni jambo la kumuumiza kichwa Saad. Lakini kwamba bado aliiendeleza tabia hiyo, ilikuwa ni kero isiyostahimilika wala kuvumilika. Bila ya kujitambua, chozi liliteleza juu ya kope na taratibu likaviringika shavuni.



    “Atakuja, na atanitambua,” kwa mara nyingine alinong'ona, sasa machozi zaidi yakitishia kububujika. Akaendelea kunong'ona, “Nitamtia makofi ya kumtosha, kisha nitamtimua na vikorokoro vyake.”



    Mara akaguna. Wazo jingine likamjia, wazo la kupinga hatua aliyotaka kuichukua dhidi ya Halima. Alichukulia kuwa kumpiga lisingekuwa jambo zuri. Ni tabia iliyokwishapitwa na wakati. Ni mambo ya kizamani. La muhimu ni kumfukuza tu. Ndiyo, amfukuze, ikibidi hata majirani wasijue, na hata watakapomuuliza atawaambia kasafiri; basi.



    Alipohitimisha zoezi la kukusanya vitu vya Halima, akaketi sofani kivivuvivu. Hazikupita hata dakika kumi mara akasikia mlango mkubwa ukifunguliwa. Akajipa imani kuwa huyo ni Halima. Lakini hisia au imani hiyo ilitiwa dosari mara aliposikia hatua za kiume zikiinyanyasa sakafu.



    Hata hivyo bado kwa mbali akaamini ni Halima, na kwamba kaamua kubadili miondoko, kawa na tahadhari, ametwaliwa na woga, au, labda aliamua kuja kiume, tayari kwa lolote; iwe kwa heri au shari.



    Taratibu Saad aliusogelea mlango wa chumba. Akasikia hatua hizo zikipita koridoni na kuishia chumba cha pili cha mpangaji mwingine. Kwa unyonge akarudi sofani na kujipweteka.

    Aliwaza jinsi Halima alivyomdhalilisha pale DDC Kariakoo.



    Maumivu yakamzidia moyoni. Sasa machozi yakamchuruzika mashavuni mfululizo na kudondoka sakafuni ta! ta! ta! Kwa haraka akayafuta machozi hayo na kutulia, akilini mwake akitumaini kuwa Halima atazuka, ataingia sekunde chache zijazo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Haikuwa kama alivyotarajia. Halima hakutokea hata ilipotimu saa 11 alfajiri, pambazuko halisi likiwa limekwishadhihirika. Kikawa ni kipindi kigumu zaidi kwa Saad. Wakati kabla ya mapambazuko alihisi njaa ikimsakama tumboni, sasa hakuihisi njaa hiyo japo alikuwa hajatia chochote tumboni zaidi ya ile soda aliyoinywa pale DDC Kariakoo jana jioni. Zaidi ni kichefuchefu kilichomsumbua.



    Isitoshe, tangu aliporejea jana, hadi alfajiri hiyo alikuwa hajaaambua hata lepe la usingizi. Kwa ujumla alikuwa hoi kimwili na kiakili.



    Alitupa macho kwenye saa ya ukutani iliyomwonyesha kuwa ni saa 11:15. Akashusha pumzi ndefu na kuendelea kutulia hapo sofani, nusu kaketi, nusu kalala. Alikuwa hatofautiani na mgonjwa mahututi. Na kwa namna moja au nyingine alikuwa mahututi.

    Hatimaye ikaja hatua nyingine ambayo hakuitarajia. Usingizi ulimpitia ghafla akiwa hapohapo sofani; nusu kaketi, nusu kalala.



    ***************



    “INATOSHA,” kwa unyonge Halima alimwambia Nsanzugwanko.

    Ilikuwa ni kauli ambayo Nsanzugwanko hakuiafiki japo aliisikia. Kwake, sauti hiyo ilikuwa nzuri, kama kinanda masikioni, ikionyesha kumhimiza aendelee kufanya alichokuwa akikifanya. Akazidisha juhudi na utundu kwa kiwango kilichoyapandisha upya 'mashetani' ya Halima kiasi cha kumfanya aungane naye kwa kukitumia kila kiungo chake katika kulifanikisha zoezi hilo.



    Wakafanya kila walichoweza, wakafanya kila walichopenda, usemi wa “mapenzi ni uchafu usiotapisha” ukidhihirika katika zoezi lao. Walitoa taswira ya waigizaji maarufu wa sinema za ngono wa Costa Rica, Brazil na Ugiriki.



    Muda mfupi baadaye walibaki wakitazamana. Kisha ghafla, Halima alimbusu Nsanzugwanko shavuni na papohapo akanong'ona:

    “Asante, mpenzi.”



    “Halima...,” Nsanzugwanko alitamka na kusita. Kwa ujumla hakujua alipaswa kusema neno gani jingine. Halima alikuwa ni mwanamke wa kipekee, mwanamke aliyemfanya ajikute akishuhudia mapambazuko pasi ya kuambua lepe la usingizi. Na hadi wakati huo bado alikuwa macho makavu na ngangari, akiwa tayari kuendelea kumfaidi Halima na vituko vyake vinavyoburudisha na kusisimua.



    Naam, aliishia kumwita tu, akaduwaa.



    “Unasemaje, mpenzi?” Halima alimuuliza.



    Bado Nsanzugwanko hakuipata sauti yake. Angeipataje ilhali tayari mikono ya Halima ilishaanza kukosa adabu na kupotea njia, hususan mkono mmoja ambao ulivuka mpaka na kutua katika uwanja halisi wa mapambano kisha ukaanza 'kufanya fujo' zilizompa mateso yasiyomuumiza?



    Angeipata wapi sauti, ilhali Halima alizidi kudhihirisha kuwa alifundwa, akafundika pale alipodiriki hata kuutumia ulimi wake kuchokonoa kila pembe aliyoiamini kuwa ndipo 'silaha' za mwanamume huyo zilipohifadhiwa?



    Hata hivyo, Halima hakuwa akihitaji chochote tena. Alisharidhika. Yote aliyoanza kumfanyia tena Nsanzugwanko ilikuwa ni katika kujiweka katika daraja la juu zaidi kwa wanawake. Ndiyo, Nsanzugwanko amchukulie kuwa ni mwanamke zaidi ya wanawake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hivyo, kama alivyouanza mchezo huo, ndivyo pia alivyouacha dakika chache baadaye. Akajitoa kitandani na kuingia bafuni kuoga. Alipotoka humo alivaa nguo na kuwa tayari kwa kuondoka. Akamfuata tena Nsanzugwanko na kumbusu shavuni. “Niombee mema huko nyumbani, mpenzi,” alimwambia.



    “Nakuombea mema. Lakini si umesema hakuna noma; unajua jinsi ya kumtuliza bwege wako?”



    Halima alicheka kidogo. “Yeah, najua jinsi ya kumtuliza. Lakini kila siku sio Jumapili au Ijumaa.”



    “Unategemea kumkuta amegeuka mbogo, si nd'o maana'ake?”



    “Inawezekana.”



    “Na kwa kuwa jana alikuona pale DDC, nakwambia hapatatosha leo huko kwenu.”



    “Patatosha tu,” Halima alisema kwa kujiamini. “Akileta za kuleta, natimua zangu. Kwetu sio mbali, ni hapo Mbagala tu. Nitakwenda. Siwezi kukaa na mwanamume asiyejua chochote...” akaiacha sentensi hiyo ikielea na badala yake akaachia kicheko kikali cha kimbea.



    Wakatazamana, ukimya ukipita kati yao.



    Mara Nsanzugwanko akanyanyuka kitandani na kulifuata begi. Akalifungua na kutoa kitita cha pesa. Akatoa fungu moja na kuzihesabu. Elfu kumi ...ishirini....hamsini...laki moja...laki moja na nusu...laki mbili. Akampatia Halima huku akiuliza, “Kwa hiyo inakuwaje? Jioni au lini?”



    Huku akipokea pesa zile, Halima alijitia kuona haya kidogo kisha akasema, “Nitakutumia meseji baada ya saa moja hivi.”



    ***************



    ALIFIKA nyumbani na kukuta mlango mkubwa ukiwa wazi. Hakushangaa kwa hilo. Baadhi ya wapangaji katika nyumba hiyo huondoka mapema alfajiri. Hivyo aliamini kuwa hali hiyo imesababishwa na uondokaji wao.



    Moja kwa moja hadi kwenye mlango uliomhusu. Alipougusa akashangaa kuona uko wazi. Akausukuma na kuingia. Macho yake yakafikia kwenye sofa kubwa. Akashtuka, mshtuko ambao haukudumu sana, akavuta hatua na kujaa chumbani humo.



    Akageukia kushoto na kumwona mumewe, Saad, akiwa sofani, nusu kaketi, nusu kalala, akimtazama kwa macho makali japo macho hayo hayakuficha athari za kukosa usingizi.



    Yalikuwa ni macho makali, ndiyo. Lakini hayakuwa tishio machoni na akilini mwa Halima. La. Yeye alimtazama Saad kama jinsi amtazamavyo kiumbe yeyote wa kawaida.



    Na katika kumwonyesha Saad kuwa yuko katika hali ya kawaida, kwa sauti ya kujiamini alimuuliza, “Vipi, mbona vurugu tupu humu ndani?”



    Ni hapo Saad alipoipata sauti yake. Aliketi vizuri sofani, na kwa sauti yenye kijimkwaruzo cha mbali, sauti iliyofurika tani kadhaa za uchungu, alisema, “Halima! Chukua vitu vyako uondoke! Tena sasa hivi!”



    “Nini?!” Halima alihoji huku kajishika kiuno.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Nadhani umeshanisikia.”



    “Kwa nini?”



    “Nasema, toka!”



    “Siondoki!” Halima aling'aka. “Siondoki mpaka un'ambie kosa langu!”



    “Nasema, ondoka!”



    “Siondoki! Labda uniue!”



    “Sitaki kukugusa, Halima,” sauti ya Saad ilikuwa ya upole.



    “Kumbuka mtoto wetu yuko kwa bibi yake. Anahitaji matunzo ya baba na mama. Nikikuua nitakuwa nimemwathiri sana mwanetu. Nakuomba tu, uondoke.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Halima alimtazama Saad kwa sekunde chache na kuibaini hasira iliyojikita moyoni mwake. Hivyo hakuhitaji kuuendeleza mjadala usiokuwa na matunda mema. Kwa upole alitwaa vitu vyake na kuondoka.

    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog