Search This Blog

Monday, October 24, 2022

TATTOO - 1

 





    IMEANDIKWA NA : NYEMO CHILONGANI



    *********************************************************************************



    Chombezo : Tattoo

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    ALIJULIKANA shuleni kama Annabel Michael. Alikuwa msichana mrembo ambaye kwa kila mwanaume aliyemwangalia alikiri kwamba katika maisha yake hakuwahi kukutana na msichana mrembo kama alivyokuwa.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Sura yake ilikuwa ya mviringo, mashavu yake yalikuwa na vishimo ambavyo hujulikana sana kama dimpozi huku pembeni ya pua yake kukiwa na kidoti cheusi kilichoufanya uzuri wake kukamilika kwa kila kitu.

    Annabel alikuwa na mvuto haswa. Sura yake ilikuwa moja ya kitu kilichowafanya wanaume wengi kutamani kuwa naye. Lipsi zake nene, macho yake ya duara na pua yake ya kisomali vilikuwa baadhi ya vitu vingine vilivyowafanya wanaume wengi kuchanganyikiwa.

    Ukiachana na sura yake, Annabel alibarikiwa kuwa na umbo zuri, hipsi zake zilikuwa zikionekana vizuri, kwa nyuma alikuwa na makalio makubwa kidogo huku miguu yake ya wastani ikiwa kitu kimojawapo kilichowafanya wanaume wengi kumtolea macho.

    Uzuri wake ulikuwa ukivuma kila siku. Wanafunzi wa shule nyingine ndani ya Jiji la Dar es Salaam walikuwa wakisikia kuhusiana na uzuri wa Annabel kiasi ambacho kila mtu akajikuta akitamani kwenda katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kisutu kwa ajili ya kumuona msichana huyo aliyesadikiwa kuwa na mvuto kuliko wasichana wote waliokuwa wakisoma na kuishi ndani ya Jiji la Dar es Salaam.

    Sifa za uzuri wake ziliendelea kutikisa jiji hilo hasa mashuleni. Annabel akajikuta akianza kupata umaarufu hata kwa watu ambao hawakuwahi kumtia machoni. Alivutia katika macho ya kila mtu aliyemwangalia, alipendeza kwa kila mwanaume ambaye alibahatika kukutana naye.

    Shule hiyo ya wasichana ikajikuta ikipokea wageni wengi kutoka katika shule nyingine za sekondari zilizokuwa ndani ya Jiji la Dar es Salaam. Ijumaa ndiyo ilikuwa siku ya michezo shuleni hapo na ilikuwa ni lazima wasichana wa hapo wacheze mpira wa wavu na timu nyingine kutoka katika shule nyingine au hata wakati mwingine wao kutoka na kwenda katika shule nyingine kwa ajili ya mechi.

    Kila walipokuwa wakiita timu kutoka katika shule fulani kwa ajili ya kucheza mechi, wanafunzi wa kiume nao walikuwa wakija na timu ya wasichana wa shule yao huku wakijifanya kutoa sapoti katika ushangiliaji kumbe lengo lao lilikuwa ni kuuona uzuri wa msichana Annabel.

    Uzuri wake haukushangawa na wavulana tu bali hata wasichana wenzake walikuwa wakimshangaa. Annabel alivutia, ngozi yake laini ya maji ya kunde iliyokuwa iking’aa kila wakati iliwavutia zaidi watu waliokuwa wakimwangalia.

    Mpira wa wavu kwa wanawake ukaanza kupata mashabiki wengi shuleni, wavulana wengi wakatokea kuupenda mchezo huo huku nyuma ya kila kitu kukiwa na uwepo wa Annabel.

    Kutokana na idadi kubwa ya wavulana waliokuwa wakivutiwa naye, maadui wa kike wakaanza kujitokeza. Wasichana hao walionekana kuumizwa na jinsi hali ilivyokuwa. Annabel alikuwa amewateka wanafunzi wengi wa kiume kiasi kilichofanya wasichana wengine kutokuwa thamani kwa wavulana, Annabel ndiye aliyefagiliwa katika kila kona.

    “Unajua toka nimekuja sijamuona Annabel!” alisema kijana mmoja, aliyekuwa miongoni mwa wanafunzi wa kiume kutoka katika Shule ya Sekondari Manzese ambao walifika shuleni hapo kushangilia timu yao.

    “Ukimuona utamjua?” mwanafunzi mwingine akauliza.

    “Nitamjua tu. Kwanza sifa yake ni uzuri, si ndiyo?”

    “Ndiyo.”

    “Basi nikimuona nitamjua tu.”

    “Una uhakika? Hapa Kisutu kuna mademu wakali mno.”

    “Nitamfahamu tu.”

    “Sawa, subiri.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Mwanafunzi huyo hakuweza kuyatuliza macho yake, kila wakati alikuwa akiangalia huku na kule, alikuwa na hamu kubwa ya kumuona Annabel ambaye kila siku alikuwa akisikia sifa za uzuri wake tu.

    Mechi ilikuwa ikiendelea lakini idadi kubwa ya wanafunzi wa kiume kutoka katika Manzese hawakuonekana kuwa makini na mchezo huo, kila wakati macho yao yalikuwa yakiangalia huku na kule kumtafuta Annabel tu.

    “Duuh! Kaka umemuona yule demu alivyokuwa mkali, nahisi ndiye yeye,” alisema kijana huyo aliyekuwa na hamu ya kumuona Annabel.

    “Demu yupi?”

    “Yule pale aliyekaa katikati ya wasichana wengine. Mmmh! Uzuri wake sijawahi kuona. Cheki mtoto alivyokuwa mkali, mtoto chotara, nywele mpaka mgongoni. Kweli leo nimeamini Annabel ni mkali balaa,” alisema kijana yule huku akimwangalia msichana huyo.





    “Duuh! Kaka umemuona yule demu alivyokuwa mkali, nahisi ndiyo yeye,” alisema kijana huyo aliyekuwa na hamu ya kumuona Annabel.

    SASA ENDELEA...

    “DEMU yupi?”

    “Yule pale aliyekaa katikati ya wasichana wengine. Mmmh! Uzuri wake sijawahi kuona. Cheki mtoto alivyokuwa mkali, mtoto chotara, nywele mpaka mgongoni. Kweli leo nimeamini Annabel

    ni mkali balaa,” alisema kijana yule huku akimwangalia msichana huyo.

    “Unamzungumzia msichana yupi?”

    “Yule pale aliyekaa katikati ya wasichana wengine.”

    “Yule aliyepakata begi jekundu?”

    “Ndiyo.”

    “Unauonaje uzuri wake?”

    “Daah! Kaka ni noma sana, yule demu matata mno.”

    “Sawasawa. Nikwambie kitu?”

    “Niambie.”

    “Yule siyo Annabel.”

    “Unasemaje?”

    “Yule siyo Annabel. Kwa Annabel, yule manzi haingii kati.”

    “Kaka acha utani. Unasema kweli yule siyo Annabel?”

    “Siyo yeye.”

    Kijana yule akaonekana kutokuamini, kila alipokuwa akimwangalia msichana yule, uzuri wake uliifanya akili yake kumwambia kwamba alikuwa Annabel. Alipoambiwa kwamba yule msichana ambaye alikuwa amemtolea macho hakuwa Annabel, tayari akaanza kukipa kazi kichwa chake na kuanza kufikiria huyo Annabel alikuwa na uzuri wa namna gani.

    Mpira ulikuwa ukiendelea, bado wanafunzi wa kiume macho yao hayakutulia, walikuwa wakimtafuta Annabel ambaye wala hakuonekana uwanjani hapo.

    Dakika ishirini kabla ya mchezo huo kumalizika, msichana mmoja mrembo akatokea mahali hapo kutoka darasani. Wanafunzi wote kutoka Manzese Sekondari waliokuwa wakitazama mpira wakageuza macho yao na kumwangalia msichana yule.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Wavulana wakabaki kimya, miguno ikaanza kusikika, utulivu ukaonekana kuanza kupotea mahali hapo, uwepo wa msichana huyo ukaonekana kuharibu kila kitu. Alikuwa Annabel.

    “Nimeamini,” kijana yule aliyekuwa akitaka kumuona Annabel alisema huku akimkodolea macho msichana huyo mrembo.

    Annabel hakuchuja, kila wakati alionekana kuwa mrembo kupita kawaida. Kwa mwendo wa madaha, akaanza kuelekea sehemu iliyokuwa na viti vya kutazama mchezo huo huku baadhi ya wasichana kutoka katika shule hiyo wakianza kukunja sura zao, mioyo yao ilikuwa ikisikia wivu kila walipokuwa wakimuona msichana huyo.

    Wavulana ambao hawakuwa wamemuona Annabel siku hiyo walimuona kwa macho yao, uzuri ambao walikuwa wameambiwa kabla waliona kama ulikuwa umepunguzwa kwa kiasi kikubwa.

    Msichana huyo alionekana kuwa mrembo hasa, kila aliyekuwa akimwangalia, moyo wake ulimthibitishia kwamba Annabel alikuwa msichana mrembo.

    “Kuna mtu anahitaji namba yako ya simu,” msichana ambaye alikuwa amekaa pembeni ya Annabel alimwambia kwa sauti ya chini.

    “Nani?”

    “Kuna mvulana kutoka Manzese Sekondari,” alijibu msichana huyo aliyejulikana kwa jina la Fatuma.

    “Hapana. Nahofia usumbufu, siwezi kutoa namba yangu ya simu. Mwambie anisamehe kwa hilo,” alisema Annabel.

    Hiyo haikuwa mara yake ya kwanza kukataa kutoa namba yake ya simu, mara kwa mara alikuwa akiwaambia watu kwamba hakuwa radhi kutoa namba yake.

    Kipindi cha nyuma, Annabel alikuwa akipokea simu nyingi kutoka kwa wanaume ambao walikuwa wakimtaka kimapenzi, walikuwa wanaume ving’ang’anizi kiasi ambacho walionekana kuwa kero katika maisha yake.

    Hali hiyo ndiyo ilimfanya abadilishe namba yake ya simu. Hakutaka kuigawa hovyo, hata baadhi ya wasichana shuleni hapo aliwanyima kutokana na kuwa na tabia ya kuiuza kwa wavulana waliokuwa wakiihitaji.

    Katika maisha yake, Annabel hakuwa msichana muongeaji sana, muda mwingi alikuwa mkimya, upole wake ndiyo ulimfanya asizoeane na wasichana wengi japokuwa alikuwa shuleni hapo kwa mwaka wa tatu.





    KILA alipokuwa akiletwa na gari shuleni, moja kwa moja Annabel alikuwa akielekea darasani ambapo huko alikaa katika kiti cha mbele kabisa na kutilia umakini kwa kila mwalimu ambaye alikuwa akiingia darasani.

    “Hatutaki kucheza na timu yoyote ile,” alisema mwalimu mkuu mara baada ya kuletewa barua zaidi ya kumi, zote kutoka katika shule nyingine ambazo zilitaka kucheza mechi ya mpira wa kikapu kwa wasichana wa shule hiyo.

    Huo haukuwa mwisho wa kuletewa barua. Mara kwa mara walimu wa shule nyingine walikuwa wakiandika barua kuja shuleni hapo kwa lengo la kucheza mechi huku nyuma ya pazia kila mtu akiwa na hamu ya kumuona Annabel.

    Siku ziliendelea kukatika. Uzuri wake bado ulikuwa ukiendelea kuvuma kila siku. Annabel akazidi kupendwa na kila aliyekuwa akimwangalia kuanzia shuleni mpaka mitaani. Wanaume walizidi kumfuata na kumwambia maneno mengi ya kimapenzi lakini Annabel hakutaka kuwaelewa.

    Pamoja na uzuri wake, fedha ambazo wazazi wake walikuwa nazo, kuna kitu kilikuwa kikimuumiza sana Annabel maishani mwake, mapenzi yalikuwa yakimtesa kama yeye alivyokuwa akiwatesa wanaume wengine.

    Kila alipokuwa akipendwa, hakuwa akipenda. Aliwatesa wanaume wengi, wengine walimfuata mpaka kumpigia magoti, kulia na hata kumuonyeshea ni jinsi gani walikuwa wakimpenda lakini Annabel hakutaka kuwakubalia kabisa.

    Kama jinsi ambavyo mapenzi yalivyokuwa yakiwatesa wengine basi hata na yeye yalimtesa vivyohivyo. Katika maisha yake akajikuta akitokea kumpenda mvulana aliyejulikana kwa jina la Jonathan, kijana aliyekuwa akisoma katika Shule ya Sekondari Mbezi, kijana huyo alikuwa na kipaji cha uchoraji.

    Kilichomshangaza Annabel, pamoja na uzuri ambao alikuwa nao, mvuto ambao alibarikiwa na Mungu, kijana Jonathan hakuwa na habari naye kabisa, kila alipokuwa akijaribu kumwambia, Jonathan alikuwa akimkataa kwa kumwambia kwamba hakuonekana kuwa na mvuto machoni mwake, hivyo ajaribu kwa wavulana wengine ambao wangeonekana kuvutiwa naye, ila kwake, Annabel hakuonekana kuwa na mvuto hata asilimia moja.

    Hicho ndicho kilikuwa kitu kilichomtesa Annabel, akajikuta akimpenda mtu asiyempenda huku wale ambao hakuwa akiwapenda, walikuwa wakimhitaji kila siku katika maisha yao.

    ***

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kila siku wanaume bado waliendelea kumfuatilia Annabel bila mafanikio yoyote yale. Uzuri wake ulikuwa gumzo kwa kila mtu ambaye alikuwa akimuona.

    Ukimya wake ambao uliwafanya watu kumhesabia kuwa miongoni mwa wasichana wazuri ukawawekea wanaume ugumu wa kumpata.

    Kipindi kizuri cha kumpata Annabel kilikuwa ni hapo shuleni au katika kipindi ambacho alikuwa akielekea katika shule mbalimbali kwa ajili ya michezo. Kila siku alikuwa akiletwa na gari shuleni hapo na kurudishwa nalo nyumbani.

    Wanaume wengi walikuwa wakisikia sifa zake lakini asilimia kubwa hawakuwa wamemuona na hiyo ndiyo ilikuwa sababu iliyowafanya wengi kuangalia kila mechi waliyokuwa wakicheza wasichana wa Shule ya

    Sekondari Kisutu kwa kuamini kwamba ilikuwa ni lazima Annabel awepo mahali hapo kama mtazamaji.

    Annabel hakuwa na muda na mtu yeyote yule, kila alipokuwa akiambiwa maneno ya mapenzi hakuonekana kuelewa kabisa.

    Hakuwa msichana wa kuleta pozi, kila mwanaume aliyeongea mbele yake alikuwa akimsikiliza lakini mwisho alikuwa akiwakataa kitu kilichowafanya wengi kumuona kwamba alikuwa msichana mwenye msimamo.

    Ni Jonathan pekee ndiye aliyekuwa ameutawala moyo wake.

    Moyo wake ukaingia katika mapenzi mazito ambayo yalianza kuchipua moyoni mwake. Japokuwa kila wakati wanaume kutoka katika shule hiyo walikuwa wakimwangalia lakini

    Annabel hakuonekana kuvutiwa nao, macho yake alikuwa ameyagandisha kwa Jonathan ambaye alikuwa akiangalia mechi hiyo huku karatasi ikiwa mkononi mwake akichora.





    “Ni mzuri mno,” alijisemea Annabel kila alipokuwa akimwangalia Jonathan ambaye alionekana kutokuwa na habari yoyote ile.



    Mpaka mechi inakwisha, Annabel alikuwa amechanganyikiwa, mawazo yake juu ya Jonathan yalikuwa yamempeleka mbali kabisa. Akajiona akitoka mtoko wa usiku na kijana huyo na kwenda katika Mgahawa wa Steers, wakanunua vinywaji na kisha kuanza kunywa.



    Muda wote huo alionekana kuwa na furaha, mawazo hayo yalimfanya ajione kwamba yupo sehemu hiyo huku akipata kinywaji pamoja na mvulana huyo aliyeonekana kuwa wa kawaida sana, shati lake lilikuwa chafu, mvulana asiyependa kuchomekea, ila alikuwa mchoraji mzuri kupita kawaida.



    “Annabel...” alisikia akiitwa, akashtuka kutoka katika lindi la mawazo, akaanza kumwangalia mtu aliyemuita, alikuwa rafiki yake, Fatuma.

    “Abeee...” aliitikia Annabel.



    “Tuondoke.”

    “Nakuja.”

    “Mbona unaonekana hivyo?”

    “Nipo vipi?”



    “Haueleweki, una mawazo sana, tatizo nini?” aliuliza Fatuma, muonekano wa Annabel ukamuonyesha kwamba hakuwa katika hali ya kawaida kabisa, alikuwa ametekwa na Jonathan kimapenzi.

    “Nipo kawaida tu.”



    “Sawa. Tuondoke, mwalimu katuita,” alisema Fatuma, kisha kuanza kupiga hatua kuelekea sehemu lilipokuwa gari la shule.



    Annabel hakuonekana kuwa katika hali ya kawaida, bado kichwa chake kilikuwa kikimfikiria mvulana ambaye alikuwa amemuona shuleni hapo, Jonathan ambaye hakuonekana kujali kama msichana huyo alikuwa shuleni hapo.



    Annabel alitumia muda mwingi sana kumwangalia Jonathan lakini mvulana huyo hakutumia hata sekunde moja kumwangalia Annabel. Hicho kilikuwa kitu pekee ambacho kilimpa mawazo sana, hakuamini kama kweli pamoja na uzuri wake uliompa sifa kwa wanaume wengi bado kungekuwa na mvulana ambaye asingeweza kutumia hata sekunde moja kumwangalia.



    Wakaingia ndani ya basi la shule. Bado Annabel hakuonekana kuwa katika hali ya kawaida. Mawazo yalikuwa yamemteka kupita kawaida, kila alipokuwa akimfikiria Jonathan alijihisi kuwa na mapenzi makubwa kwa kijana huyo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Annabel, una nini leo?” aliuliza Fatuma.

    “Hakuna kitu.”

    “Hapana. Kuna kitu, hebu niambie.”

    “Hakuna kitu Fatty.”

    “Sawa.”



    Annabel hakutaka kuwa muwazi, kila kitu ambacho kilikuwa kikiendelea moyoni mwake alitaka kukifanya kuwa siri. Hakutaka mtu yeyote afahamu kile kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake, hakutaka kumwambia Fatuma kwamba kulikuwa na mvulana ambaye alitokea kumpenda, mvulana ambaye alimfanya ajisikie wa tofauti sana moyoni mwake.



    Kuanzia siku hiyo Annabel akawa katika hali ya mawazo, mara kwa mara alikuwa akimfikiria Jonathan ambaye mpaka katika kipindi hicho hakuwa akilifahamu hata jina la mvulana huyo.



    “Nitampata vipi? Natamani kumwambia ukweli, nimetokea kumpenda. Mungu wangu! Mbona mapenzi yanakuwa hivi, nitamwambia ukweli tu. Lakini lini? Lini tutarudi Mbezi High School? Nitamfuata, siwezi kuvumilia kabisa,” alijisemea Annabel.



    Upweke moyoni mwake haukukoma, kila siku alikuwa akimfikiria mvulana huyo ambaye aliuteka moyo wake. Kiukweli alimhitaji sana, hakutaka kuwa na mwanaume mwingine yeyote zaidi ya Jonathan ambaye hakuwa na taarifa kama alikuwa akipendwa na msichana huyo aliyekuwa akisifika kwa uzuri katika sehemu mbalimbali ndani ya Jiji la Dar es Salaam.



    “Nataka unisaidie kitu Fatuma,” Annabel alimwambia Fatuma ambaye alimsogelea karibu.

    “Kitu gani?”

    “Unakumbuka siku ile tuliyokwenda kule Mbezi High School?”

    “Ndiyo nakumbuka.”

    “Kuna kitu.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Kitu gani?”

    “Kuna mvulana nilimuona.”

    “Mvulana yupi?”



    “Sijui ni mvulana yupi.”

    “Sawa. Amefanya nini?”



    ITAENDELEA 

0 comments:

Post a Comment

Blog