Search This Blog

Monday, October 24, 2022

GUBERI LA KIMANYEMA - 5

 





    Chombezo : Guberi La Kimanyema

    Sehemu Ya Tano (5)



    Aliporudi hotelini alijiandaa kwa safari hiyo akidhamiria kukabidhi chumba kabla ya saa 10 jioni ili Suzy asimkute hapo. Naam, kila jambo lilitekelezwa kwa jinsi alivyopanga.

    Akaikimbia Dar es Salaam.

    *****

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    SIKU ya tatu, saa 2 asubuhi treni iliingia mjini Kigoma. Kiwembe alipoikanyaga ardhi ya mji huo tu, akahisi ikimsuta. Alipokutanisha macho na baadhi ya waliofika hapo stesheni kuwapokea jamaa zao, akayaona macho yao kama vile yakimdhihaki.

    Lakini angefanya nini? Jiji la Dar es Salaam ndiyo alishaliona kuwa halitofautiani na ikulu ya Jehanamu. Ni jiji lenye raha za kishetani na wakazi wenye mioyo ya kishetani. Lilikuwa ni jiji ambalo zaidi ya kuliona kuwa limemkinai, pia lilimtisha na akaliogopa kama kifo.

    Alizaliwa Ujiji, akakulia Ujiji. Ujiji ndiyo asili yake. Atakimbilia wapi tena? Atakimbilia wapi wakati alitambua fika kuwa hata aliijua dunia ya mapenzi akiwa hapohapo Ujiji?

    Ndiyo maana asubuhi hii alipokiacha kituo cha treni cha Kigoma mjini, alikodi teksi iliyompeleka ndani ya kitongoji cha Ujiji katika eneo moja lililoitwa Kasingirima. Madhumuni ya kuelekea huko Kasingirima yalikuwa ni kufikia kwa Mama Kadala.

    Na alipofika alimkuta akiandaa vyakula vya wateja wake. Ile kazi yake ya ‘Mama Lishe’ bado alikuwa akiendelea nayo huku pia akiwa bado anaendelea kupakata dogodogo.

    “Haa! Kiwembe!” alibwata mara tu alipomwona Kiwembe akishuka kwenye teksi. Kwa ujumla hakuyaamini macho yake. Akaacha kila alichokuwa akikifanya na kumkodolea macho.

    Kisha akaongeza, “Jamani hivi ni wewe kweli au naota?”

    “Huoti, mama. Ni mimi.”

    “Hapana, wewe sie Kiwembe…”

    “Ni mimi mama,”Kiwembe alisema huku akitua begi chini. “Kwanini huamini?”

    Mama Kadala alihema kwa nguvu, mikono kaikita kiunoni, akiendelea kumtazama Kiwembe mithili ya atazamaye mzimu. Kisha kwa sauti ya kusitasita akasema, “Haya, karibu. Karibu mpenzi wangu wa zamani.”

    Akalitwaa begi lake na kuliingiza ndani. Sasa uchangamfu ukamrudia. Akaonekana mwenye furaha kiasi cha kumtia woga Kiwembe. Haikumwingia akili kuwa Mama Kadala anaweza kumpokea tena, achilia mbali kumpokea kwa uso wenye bashasha ilhali alipoondoka waliagana kwa mtafaruku mkubwa.

    Hata hivyo woga wake ulizidi kupungua kadri muda ulivyokwenda mbele kutokana na jinsi alivyozidi kukirimiwa kama mgeni wa heshima.

    Mama Kadala aliharakisha kumchemshia maji ya kuoga na kuyapeleka bafuni. Alipokwishaoga akakaribishwa chumbani ambako alikuta chakula kwa ajili yake.

    Wakati akila Mama Kadala alimjia na kumwambia, “Haya mwenzangu, mi’ nd’o natoka ivo. Kazi yangu ya U-mama n’tilie sijaiacha, hivyo nawawahi wateja wangu.”

    Alipokwishasema hivyo aliinama na kumbusu katika shavu la kulia na kuongeza, “Jisikie nyumbani. Usihofu kitu. Ukijisikia upweke sana, fungua droo ya ile kabati ndogo sebuleni utaikuta rimoti ya tivii. Nadhani ukiwa unaangalia angalia tivii upweke utapungua kwa kiasi fulani.”

    Kiwembe alipobaki peke yake, mawazo yakamrudia. Kwanza aliona kama vile ni ndoto tu iliyomtokea. Ndoto yenye yote mazuri ya kupendeza na yote mabaya ya kuchukiza na zaidi, yote ya kutisha.

    Je, haya nayo ya kupokelewa na Mama Kadala ni mazuri? Kama haya ni mazuri, je, mabaya ni yapi? Mtu ambaye walitimuana kwa kosa lisilosameheka, leo anampokea kwa uchangamfu mkubwa na huduma nzuri kiasi hiki. Je, hakuna jambo baya lililojificha nyuma ya wema huo?

    Hakuamini.

    Hata alipomaliza kula na kujitupa sofani, bado aliendelea kukitaabisha kichwa kwa kuwaza hili na lile kuhusu Mama Kadala. Mawazo hayo yaliendelea hadi usingizi ukamteka taratibu, usingizi uliosababishwa na uchovu wa safari sanjari na shibe nzito ya stafutahi.

    *****

    MAMA Kadala alirejea saa moja jioni na kumkuta Kiwembe palepale sofani akiwa ametopea usingizini. Akashangaa na kumtazama kwa muda. Kisha akatua chini vyombo vyake vya kazi. Akajifunga kanga vizuri kiunoni na kumsogelea. Akamtikisa polepole hadi Kiwembe akazinduka.

    “Enhe, vipi tena?” alimuuliza kwa mshangao. “ Inakuwaje ulale hapa sofani ilhali kitanda kipo? Amka basi ule kwanza. Usiku umeingia.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Asante sana mama, bado nimeshiba,” Kiwembe alijibu kivivuvivu huku yale mawazo yake kuhusu tukio la Magomeni Mikumi yakimrudia kichwani.

    “Haya, kama huli hamia basi kitandani,” Mama Kadala alimhimiza huku naye, bila ya haya, akachojoa nguo zake zote na kubaki mtupu kama wapendavyo watu wa aina yake.

    Halikuacha vituko jimama hilo, guberi la Kimanyema! Akatwaa khanga na kujifunga kifuani.

    Kiwembe alishuhudia yote hayo, lakini noyo ulimdunda kwa nguvu kila alipolifikiria lile tukio la Magomeni Mikumi jijini Dar es Salaam.

    ‘Sijui yaliyonifika ni kweli?’ alijiuliza kimoyomoyo huku akinyanyuka kutoka kitini. Lakini itakuwa vipi KWELI iwapo hajahakikisha? Akajipa moyo wa matumaini huku akipanda kitandani.

    Ni wakati huo alipovuta kumbukumbu ya vituko vya Mama Kadala, vituko alivyomfanyia muda mfupi uliopita. Akakiri kuwa maisha yalimkubali Mama Kadala. Unene wake ulikuwa uleule, lakini sasa alinawiri zaidi huku tako lake likitishia kupasuka. Kwa ujumla alipendeza machoni mwa Kiwembe, zaidi ya kipindi kile, enzi za uhusiano wao.

    Japo sasa Mama Kadala alipendeza zaidi na kuwa na mvuto mkubwa mbele ya mwanamume yeyote mwenye uchu wa ngono, kwa usiku huu wakiwa wamejifunika shuka moja, miili yao ikigusana na kupeana joto, bado maungo ya Kiwembe hayakupata mshtuko wowote!

    Walilala hivyo hadi kunakucha, wakiwa hawatofautiani na ‘Zainabu na Zinduna.’ Siku iliyofuata hali ikawa hiyo hiyo. Kiwembe hakuwa yule Kiwembe ambaye ni kiasi tu cha kuiona sehemu ndogo ya paja la mwanamke basi ‘moto’ unamwakia. Huyu alikuwa Kiwembe aliyepoa, Kiwembe asiyeweza lolote.

    Hata hivyo Mama Kadala akahisi kuwa huenda labda ni woga au kwa kuwa siku nyingi hawajaonana na kwa kuwa pia waliachana kwa kutimuana. Kwa siku hiyo akamsamehe.

    Asubuhi ya siku ya tatu Kiwembe aliamka huku akiwa ametingwa na mawazo tele kichwani. Kwa ujumla alichanganyikiwa. Akajiuliza maswali mengi kuhusu Mama Kadala.

    Baadhi ya maswali hayo ni je, mama huyo hatashangaa kumwona kijana huyu wa kiume aliyemfundisha zoezi la kimwili, akawa mtaalamu, kabla ya kukumbwa na kichaa cha mapenzi, anashindwa kuonesha uwanaume wake usiku huu?

    Je, kusafiri katika treni kwa siku tatu kutoka Dar es Salaam hadi Kigoma huweza kuwa sababu tosha ya kumfanya mwanamume akumbwe na uchovu kwa siku mbili mfululizo baada ya safari, kiasi cha kushindwa hata kufanya tendo la ndoa japo kwa dakika tano tu?

    Aliamini kuwa Mama Kadala atajiuliza mengi, na kati ya hayo mengi, hayo mawili yatakuwa miongoni. Alitambua jinsi mama huyo anavyokuwa mkorofi pindi anapokerwa na jambo lolote. Na aliamini kuwa tayari ameshakerwa na hali hii iliyotokea kwa siku mbili mfululizo.

    Akakumbuka kuwa jana, usiku wa manane, akiwa usingizini, alihisi mkono ukimpapasa katika sehemu zake za siri. Alizinduka taratibu na kugundua kuwa haikuwa ndoto bali Mama Kadala alikuwa akihitaji.

    Mkono huo ulifanya kile ambacho kwa siku za nyuma, kabla ya mkasa wa Magomeni Mikumi, kingekuwa kimeshamchanganya Kiwembe kwa kiwango cha juu. Lakini kwa usiku huo, Kiwembe hakuhisi msisimko wowote!

    Tangu alipopanda kitandani usiku wa siku hiyo ya tatu, moyo ukawa ukimdunda kwa kasi kila ilipotokea Mama Kadala akamgusa. Alikuwa na mchecheto mithili ya bwana harusi aliyesikia kuwa mchumba wake yu bikira.

    Hali hiyo ilimkasirisha sana mama mwenye nyumba, Mama Kadala. Akaupeleka mkono hadi kwenye swichi na kuwasha taa. Chumba chote kikaenea nuru kali ya globu ya umeme. Akamtazama Kiwembe kwa jicho kali huku akihema kwa nguvu. Kisha: “Haya, vipi, imekuwaje tena mwenzangu?”

    “Nimerudi, mama. Nimerudi tuishi.” Ndilo jibu lililotoka kinywani mwa Kiwembe.

    “Tuishi?!” Mama Kadala alimtazama kama atazamaye uchafu jalalani. Akaongeza sauti kidogo, “Unasema umekuja tuishi?”

    “Ndio, mama.”

    “Tuishi mimi na wewe katika hali hii?” Mama Kadala alimaka.

    Mara ghafla, akacheka. Hakikuwa kicheko chenye taswira yoyote ya furaha, hapana. Hiki kilikuwa kicheko cha mchanganyiko wa hasira na dharau. Na kwa jinsi alivyomtazama Kiwembe huku akiwa ameibibitua midomo yake, ilitosha kudhihirisha kuwa amemdharau kwa kiwango kikubwa.

    Mama Kadala alimkodolea macho yake makali.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Tuishi kama Mwanahamisi na Mwanaidi au mwanamume na mwanamke?” hatimaye alirusha swali huku akiendelea kumtazama Kiwembe mithili ya atazamaye chochote kile kisichopendeza.

    Lilikuwa ni swali lililouchoma vilivyo moyo wa Kiwembe. Hasira zikamfura kifuani, akatweta mithili ya chura aliyeona nyoka aina ya Kifutu. Akamtazama Mama Kadala kwa macho makali yasiyopepesa.

    Haikusaidia kitu!

    Punde akahisi nguvu zikimwishia. Awali alikuwa hajaamini kuwa lile tukio la Magomeni Mikumi lilikuwa la kweli, lakini sasa aliamini. Siku tatu alizolala na Mama Kadala, usiku kucha bila ya kufanya lolote zilitosha kumpa picha halisi kuwa sasa siyo dume la kujivuna mbele ya watu.

    Amehasiwa!!

    Aliamini hivyo. Unyonge na simanzi wakawa wafalme wa nafsi yake. Kwa kiasi fulani akawa robo tatu ya mwendawazimu.

    “Ikiwa itawezekana mama, basi unifanye house boy wako,” Kiwmbe alisihi.

    Ilikuwa dhahiri kuwa alitamka hivyo bila ya kupima uzito wa tamko lake.

    Alishachanganyikiwa!

    Mama Kadala alimkodolea macho yake makali, akimtazama kwa dharau isiyo kifani. “House boy? House boy au house girl?” hatimaye alibwata huku akibibitua midomo na pua mithili ya anusaye uvundo wa mzoga.

    Hilo likawa ni tamko lililomkera zaidi Kiwembe. Lilipenya masikioni mwake mithili ya radi iliyopasua mawingu, na kutua moyoni kama kaa la moto. Na kile kitendo cha Mama Kadala kubibitua midomo na pua kilimfedhehesha sana kiasi cha kujikuta akipoteza ule uvumilivu wake.

    Akafoka: “Acha kashfa we Mama Kadala! Acha kabisa! We’ ni Malaya! Malaya mkubwa! Jitu zima, jimama lenye vijukuu eti sasa unajibaraguza wakati ni wewe uliyeyasababisha yote haya. Sasa unafurahi kuniona hivi?”

    Akatulia na kuendelea kumtazama Mama Kadala kwa macho yenye kilo mia moja za hasira nyuma yake. Cha ajabu Mama Kadala hakuonyesha kushtushwa na maneno makali ya Kiwembe. Alirejea kubibitua midomo kisha akatema mate chini, pwaa!

    Naam, Mama Kadala, jimama lenye sura ya kuvutia, mwili mkubwa na teketeke uliong’ara, jimama lenye macho baridi halikuwa na wasiwasi wala mshtuko wowote.

    “Siku ile uliponilazimisha penzi nisilolijua, kumbe ulikuwa ukiniwangia!” Kiwembe alimaka. “Haya si ndiyo uliyoyataka? Ukanilazimisha mambo nisiyoyafahamu hata nikabalehe kabla ya wakati wangu! Sasa leo unan’kana? Kumbe ulidhani yakinikuta ya kunikuta nikimbilie wapi kama sio kwako?”

    “Kwangu?” Mama Kadala alifyatuka. Hakujali maneno ya mwanzo aliyoambiwa na Kiwembe, alijali ya mwisho. “Toka! Toka! Nasema, toka! Toka sasa hivi mbwa koko we! Mimi! Mimi nikiwa ni Mama Kadala mwenye akili timamu na damu ikinichemka kama kawaida, kamwe siwezi kulala na mwanamke mwenzangu kitanda kimoja kwa siku tatu mfululizo! Siwezi, na sitaweza! Wallah nakuapia!”

    Maneno hayo yalikuwa ni karipio jipya, tishio, fedheha, aibu na dharau kwa Kiwembe. Yalimwingia na kumchoma mithili ya aliyemeza kisu na sasa kilikuwa kikimkatakata utumbo. Akahisi tumbo la kuharisha. Akatetemeka mwili mzima mfano wa mzuka uliopandisha mashetani.

    Hawakuishia maneno tu; walidiriki kurushiana makonde mazito, wakigaragazana huku wakiwa tupu kama walivyozaliwa. Vita hivyo vilivyoanzia kitandani sasa vikashuka sakafuni.

    Kofi kali alilotwishwa Kiwembe, lilimyumbisha mara mbili kabla halijampeleka sakafuni akitanguliza pua tii! Pua hiyo ikachubuka na kuzua maumivu makali mwilini mwake. Hasira zikampanda maradufu, hasira zilizompandisha mori wa kunyanyuka haraka ili amfunze adabu Mama Kadala.

    Hakufanikiwa!

    Mama Kadala alikuwa na mwili mkubwa na pia alikuwa mwepesi ajabu, wepesi usiotofautiana na paka mwenye njaa. Tayari alishamfikia Kiwembe pale sakafuni na kumkandamiza, uzito wa mwili wake ukiwa ni nyenzo tegemezi.

    Kiwembe alihisi kuwa kulikuwa na hatari ya kutolewa roho na guberi hilo la Kimanyema, guberi ambalo sasa lilionyesha dhahiri kufanya lolote katika kuilinda hadhi yake. Mama Kadala aliendelea kumkandamaiza, akiisaka shingo yake.

    Kiwembe akaamua kujitutumua. Akatumia nguvu zake zote, akaikaza misuli na kunyanyuka kwa nguvu, akamtupa Mama Kadala chini kwa kishindo puu! Naam, Mama Kadala na mwili wake mkubwa akatupwa sakafuni kama gunia la mashudu.

    Hata hivyo bado ule wepesi wa Mama Kadala ulikuwa palepale! Akanyanyuka haraka, akaifuata kabati huku akihema kwa nguvu mithili ya nguruwe pori. Akafungua mlango wa kabati ambako alitoa upanga ulionolewa kwa umeme.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “N’takuua… n’takuua mwanaharamu wee…n’takuua nakwambia,” alifoka. “Toka! Toka nyumbani kwangu! Waliokutia uhanithi umewaacha, sasa unataka kuja kufia kwangu! Toka!”

    Naam, Mama Kadala alionyesha dhahiri kutokuwa na mzaha. Alipunga upanga huku akimsogelea Kiwembe. Macho yake meupe, madogo yalimwangalia Kiwembe kwa dalili zote za kuua. Dalili hizo zikatoa picha halisi muda mfupi baadaye. Kiwembe alikoswakoswa panga la kisogoni.

    Hilo likawa ni tendo lililomzindua Kiwembe. Papo hapo akarusha teke lililogota kwenye mkono wa kulia wa Mama Kadala, mkono uliokuwa umeshika upanga. Upanga ukamtoka, na zaidi Mama Kadala mwenyewe akateleza na kuanguka kifudifudi sakafuni.

    Kwa uchungu na hasira za tangu kule Magomeni Mikumi jijini Dar es Salaam hadi hapa Ujiji, Kigoma mjini, Kiwembe hakuwa na muda wa kutafakari athari au uzuri wa hatua yoyote atakayochukua dhidi ya yeyote atakayekuwa ‘chizi’ mbele yake.

    Alilitwaa lile panga na kulishusha kwenye makalio ya Mama Kadala kwa namna ya kufyeka pyuu!

    Pande la nyama likaruka likifuatiwa na mmiminiko wa damu nyingi kutoka kwenye jeraha.

    “Yalaa..! Yalaa!..Nakufa…! uwiii! Jamani nakufaaaa!” Mama Kadala alipiga yowe kali lililovuka kuta za chumba hicho, likavuka nyumba hiyo na kwenda kutua kwenye masikio ya majirani.

    Muda mfupi baadaye umati wa watu ukafurika nje ya nyumba hiyo. Wakausukuma mlango.

    Haukufunguka!

    Subira haikuhitajika. Wakaupiga nyundo na shoka.

    Ukapasuka vipande viwili!

    Watu wanne, wanaume wa shoka wakaingia kwa kishindo. Walichokishuhudia kiliwaduwaza kwa sekunde moja, sekunde ya pili jazba zikawapanda. Mmoja akamfuata Kiwembe na kumkwida shingoni.

    Tofauti ya nguvu, uwezo wa kufikiri haraka na kuchukua uamuzi bila ya kuchelewa ilimsaidia Kiwembe. Aliupangua mkono ule ulioanza kulifinya shingo lake, na papohapo akamvurumishia mtu huyo konde zito la shingoni, konde lililomtupa chini sawia.

    Lilikuwa ni tukio la ghafla, la muda mfupi sana lakini liliwashangaza na kuwaachia maswali mengi wale walioingia na mtu huyo. Kati yao hakuna ambaye aliujua uwezo wa mtu huyo katika vurugu. Aliitwa Jitu, na hakuwa mtu wa kawaida.

    Umbo lake la kikakamavu, refu lilimtisha kila amtazamaye. Na siyo mwonekano pekee wa umbo lake uliowafanya watu wamwogope, la. Historia yake.

    Alishaua watu kadhaa kwa mkono wake wa kushoto. Alishapambana na watu saba na akawashinda bila ya watu hao kufanikiwa kumtupa chini walao mara moja!

    Leo Jitu anapokea konde moja tu! Konde hilo linamtupa sakafuni! Wenzake walishangaa, na wakati wakiwa katika mshangao huo, walikumbwa na tukio jingine lililowazidishia mshangao vichwani mwao.

    Kiwembe hakuwapa muda wa kufanya chochote, alilitwaa panga na kulipunga hewani, kushoto na kulia huku akisogea mlangoni. Nani angemzuia? Njia ikawa nyeupe.

    Akatokomea gizani.

    Mbio zake hazikuwa za kumpeleka mbali kama alivyotarajia. Alipozuka mtaa wa pili, akiwa na lile panga mkononi, akakutana na kundi la vijana zaidi ya kumi wakiwa katika lindo la sungusungu. Panga likamponza.

    “We! Simama!” mmoja wa walinzi hao wa mtaa alimzuia.

    Kiwembe akaiona hiyo ni nuksi kubwa. Akaliinua panga juu akitishia kulishusha mwilini mwa kijana huyo, akiamini kuwa hiyo ni njia mojawapo ya kujihami.

    Lakini lengo lake halikufanikiwa. Mkono wake ulidakwa kijasiri na kijana huyo.

    “Mwizi!” Kijana mwingine alipiga kelele.

    “Ua!” mwingine tena akabwata.

    Tayari kundi zima lilishamzunguka Kiwembe, kila mmoja akiwa na kiu naye.

    “Mchinje!”

    “Fyeka korodani zake!”

    “Mwacheni awe mke wetu usiku huu!”

    Yalisemwa mengi, hasira zikiwa bayana katika sauti zao. Dakika tano zikakatika, mzozo ukiendelea na kushindwa kufikia mwafaka ni adhabu ipi iliyomstahili. Na wakati huo tayari Kiwembe alishapambuliwa nguo zote na kuachwa mtupu.

    Ni Sheikh Suleiman Haji aliyetoka ndani mwake baada ya kusikia mtafaruku huo ndiye aliyemnusuru Kiwembe. Heshima aliyokuwa nayo mzee huyo katika jamii iliyomzunguka ndiyo iliyowafanya vijana hao wayasikilize mapendekezo yake.

    Aliwataka vijana hao kutochukua sheria mikononi, na kwamba kama kuna tuhuma yoyote inayomhusu Kiwembe basi, vyombo vya dola vichukue mkondo wake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kauli yake iliheshimika. Kiwembe akapelekwa kituo cha Polisi. Huko akatuhumiwa kukutwa na panga lililotapakaa damu, na kushukiwa kuwa ametoka kufanya uhalifu.

    Dakika chache baadaye umati mkubwa watu ukafika kituoni hapo. Ndipo tuhuma za kumjeruhi Mama Kadala zikampata. Uzito wa kesi ukamwelemea. Ikawa ni kesi iliyomkalia vibaya. Akajikuta akihukumiwa miaka hamsini jela kwa kosa la kukusudia kukuua.

    Jeraha la Mama Kadala lilimfanya alazwe wodini hospitali ya Maweni zaidi ya miezi miwili na alipotoka hakuweza kufanya kazi kama kawaida. Mwanaye, Sharifa akatwaa nafasi ya kutoa huduma ya Umama ntilie huku akimtunza mama yake.



    ***SEMA LOLOTE KUHUSU SIMULIZI HII***

    MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Blog