Search This Blog

Monday, October 24, 2022

JASHO LA MASUMBUKO - 1

 





    IMEANDIKWA NA : INNOCENT A. NDAYANSE (ZAGALLO)



    *********************************************************************************



    Chombezo : Jasho La Masumbuko

    Sehemu Ya Kwanza (1)



    KAMA ingetokea ukabahatika kukutana naye, katu usingeyabandua macho yako mwilini mwake. Alijaaliwa macho yaliyostahili kupewa hadhi ya macho 'yanayoshawishi' na kusisimua. Na alikuwa na umbo zuri, umbo alilojua kulitumia vilivyo. Naam, lilikuwa ni umbo lililojengeka kike.



    Mtazame jinsi anavyotembea, akijitupatupa kwa madaha. Hana wasiwasi mtoto wa kike. Hutaridhika kumtazama mbele tu, la hasha. Kwa vyovyote lazima nafsi itakushinikiza umtazame mgongoni, na hapo ndipo utakapokiri kuwa umebahatika kumwona mrembo, zaidi ya warembo.



    Huenda hata kama wewe ni miongoni mwa walimu wagumu sana kutoa alama zao, kwa binti huyu utakuwa huna ujanja. Si ajabu ukajikuta ukitoa 'mpya' kwa kumpa alama zaidi ya mia moja, kinyume na misingi ya utahini katika taaluma ya ualimu.



    Kabla ya Masumbuko hajakutana na mrembo huyo, alikuwa na msimamo tofauti. Aliwadharau sana waandishi wa hadithi, makala mbalimbali magazetini na hata mashairi, waliopoteza muda wao mwingi wakijaribu kuusifia uzuri wa mwanamke. Aliwaponda na kuwaona ni watu walioishiwa ubunifu na pia ni wadhalilishaji wa jinsia.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Lakini tangu amwone mrembo huyu, msimamo wake juu ya wanawake ulibadilika. Sasa aliamini kuwa ni kweli kuna wanawake wazuri duniani, wanawake walioumbwa kwa vipindi maalumu vya kihistoria, vipindi ambavyo Mwenyezi Mungu aliamua kuwakumbusha binadamu juu ya utukufu na uwezo wake. Na hapo ndipo alipomteremsha kiumbe mahsusi kama huyu.



    Zipo tetesi ambazo bado hazijathibitishwa rasmi, kwamba, wakati wa kuumbwa kwa viumbe wa aina hii, Mungu alikesha usiku kucha akichora ramani za sura na miili yao katika jalada lake kubwa la kumbukumbu za uumbaji, jalada ambalo shetani alijitahidi kulipora bila ya mafanikio.



    Baada ya siku nyingi za mkesha wa kazi ngumu, muumba mwenyewe akiandamana na malaika wenye vyeo vikubwa, alishuka na kuwabariki wazazi wa viumbe hao siku mimba zilipotungwa.



    Inasemekana kuwa siku ya kuzaliwa kwa warembo hao, muumba alizoea kustarehe na kufurahia matunda ya kazi yake ya uumbaji. Sherehe kubwa hufanyika huko mbinguni ambako muumba alitoa zawadi nyingi ikiwa ni pamoja na kuwapandisha vyeo malaika walioshiriki kikamilifu katika ufanikishwaji wa zoezi hilo.



    Hapy ni tokeo halisi la mpango huo, mpango ambao Mungu alidhamiria kuudhihirishia ulimwengu kuwa yeye ni msanii mkuu na wengine ni waigaji tu. Naam, Happy alikuwa ni mzuri kupindukia. Ni vigumu kwa mchoraji au mwandishi yeyote duniani kuuelezea uzuri wa Happy bila ya kumdhulumu, zaidi atahukumu.



    **********

    NZEGA, moja ya wilaya zilizokamilisha mkoa wa Tabora ndiko Masumbuko alikoishi. Pia, ndiko alikoishi Happy. Masumbuko na Happy walifahamiana na kuzoeana kwa kuwa walisoma pamoja; shule moja na darasa moja.



    Kati yao hakuna aliyejua jinsi ilivyotokea hata wakazoeana hatimaye kuunda urafiki, urafiki ambao Masumbuko hakuwa na uhuru nao. Kwa ujumla hakujiamini.



    Happy alikuwa ni mtoto kigori na mrembo sana aliyezaliwa katika familia ya kitajiri. Baba yake, Mzee Mkombo alikuwa ni daktari bingwa wa mifupa. Baada ya kuhitimu elimu ya udaktari huko nchini Urusi aliingia mkataba na hospitali moja kubwa ya jijini Johannesburg, Afrika Kusini.



    Ni huko Johannesburg alikojipatia pato ambalo pindi aliporejea Tanzania alikuwa ni miongoni mwa wale waliokwishaufukuza umaskini.



    Akafungua hospitali zake tatu; moja, Tabora mjini; ya pili, Sikonge; na nyingine; Urambo. Pia alikuwa na mifugo mingi iliyomwongezea hadhi na heshima mbele ya jamii.



    Ni umaarufu huo wa Mzee Mkombo ambao huenda pia ndio uliomwongezea umaarufu mtoto wake, Happy. Kila Happy alipopita mitaani, watu walinong'onezana: “Unalicheki toto la dokta Mkombo? Toto limekamilika kila idara. Lina sura nzuri na umbo zuri vilevile.”



    Naam, ni umaarufu huo, na uzuri huo uliomfanya Masumbuko ajihisi kutowiana na Happy hata kwa maongezi ya kawaida. Masumbuko alizaliwa katika ukoo duni, na hata mwonekano wake ulidhihirisha hivyo.



    Lakini, pamoja na ufukara wake bado Happy alionyesha kumjali. Mara kwa mara walitembeleana. Urafiki wao ukakua na hatimaye ukakomaa hata ukawafikia wazazi wao kiasi cha wao pia kuwa na ukaribu kufuatia ukaribu wa watoto wao.



    Kwa hali hii haikuwa ajabu kwa Masumbuko kumsaidia Mzee Mkombo kuwapeleka mbuzi malishoni kila jioni alipotoka shuleni. Na kwa kuwa alishazoeana na Happy ikawa hata huko malishoni huwa pamoja wakizungumzia mada hii na ile hususan kuhusu masomo.



    Lakini pamoja na hayo, bado Masumbuko hakujiamini. Alikuwa na chembechembe za woga dhidi ya Happy. Haikuwa kumwingia akilini kuwa urafiki wao ungeweza kufikia kiwango walichofikia.



    Msichana mzuri kama Happy, tena ni mtoto wa tajiri, daktari bingwa; na mvulana mchafu kutoka katika ukoo wa kimaskini, muungano utoke wapi? Kwa hali hiyo, kama volkano itokotayo chinichini, Masumbuko aliendelea kuumia kimyakimya.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Ilitokea kiasi kwamba hata wale wavulana, hususan watoto wa matajiri wengine, wavulana ambao Happy hakuwa radhi kujihusisha nao hata kwa maongezi ya kawaida waanze kumdhihaki Masumbuko. Baadhi yao walidiriki kumwambia kuwa eti alimroga Happy ili ampende.



    Dhihaka hizo zilimuumiza sana Masumbuko. Hivyo, siku moja jioni wakiwa huko malishoni, Masumbuko alimwambia Happy kuhusu dhihaka hizo.



    Ilikuwa ni taarifa iliyomshangaza sana Happy. Akamtazama Masumbuko kwa makini kisha akasema, “Achana nao, Masumbuko. Waache waseme lakini si usiku watalala? Kama wangekuwa wanatusema mchana kutwa na usiku kucha, labda ingenishangaza na kuniumiza. Duh, jamani yaani hata urafiki wa kawaida imekuwa nongwa?”



    “Lakini Happy,” Masumbuko alisema, “kwa kweli sifurahii kudhihakiwa hivyo. Ni bora urafiki wetu uvunjike. Kama ni umaskini wangu unaowafanya hao watoto wa matajiri waninyanyase kiasi hiki, basi ni bora urafiki wetu ufe, nibaki na umaskini wangu. Siwezi kuuepuka ufukara ulioigubika familia yetu. Ni Mungu aliyewapa wao ndiye pia aliyeninyima mimi.”



    Happy alikunwa vilivyo na maneno hayo. Akamtazama Masumbuko kwa makini. Akaigundua simanzi iliyojikita moyoni mwa Masumbuko kiasi cha kujitokeza usoni. Huruma ikamwingia. Akainamisha uso chini. Akashindwa kuyazuia machozi yaliyojiunda machoni mwake kiasi cha kutiririka mashavuni.



    Masumbuko aliyaona machozi hayo. Akamsogelea na kumgusa kichwani. “Unalia nini, Happy?” alimuuliza.



    Happy hakujibu. Alianza kuyafuta machozi kwa kutumia kanga aliyojifunga kiunoni.



    “Happy, una nini?” Kwa mara nyingine Masumbuko alimuuliza huku akimshika mkono.



    Bado Happy hakujibu, na zaidi aliunyofoa mkono ulioshikwa na Masumbuko kisha akaketi chini.Akaishika tena kanga yake na kurudia kujifuta machozi.



    Kama awali, Happy hakujibu. Zaidi, safari hii alimvuta Masumbuko na kumkandamiza kifuani pake huku akiachia miguu yake, mmoja huku na mwingine huko. Lilikuwa ni tukio ambalo Masumbuko hakulitarajia. Lilitokea ghafla. Masumbuko akajikuta akimwangukia na kumlalia.



    Happy hakuonyesha kujali, alimkumbatia zaidi, macho kayafumba.



    Lakini mara Masumbuko akazinduka. Akaikwanyua mikono ya Happy na kuinuka. Kwa wasiwasi akaangaza macho huku na huko.

    Kwa mbali akawaona wanawake wawili wakielekea kuteka maji kisimani. Akainama na kumnong'oneza Happy sikioni: “Amka. Kuna watu wanakuja. Tutapanga siku nyingine.”



    Happy alielewa. Akainuka na kuondoa nyasi kichwani, Masumbuko akimsaidia kuziondoa mgongoni. Walirudi nyumbani kimyakimya.



    **********



    USIKU wa siku hiyo Masumbuko hakupata usingizi mapema. Kila alipofumba macho, alihisi anamwona Happy amelala chali huku kayaziba macho kwa viganja vyake laini. Ndiyo, usingizi ulimpaa Masumbuko. Akawa akijigeuzageuza katika ngozi ngumu ya ng'ombe iliyokuwa juu ya kitanda kichakavu cha miti. Juu ya kitanda hicho ndipo ilipokuwa hiyo ngozi ngumu ya ng'ombe ambayo aliilalia.



    Ni wakati macho yakiwa yameanza kuwa mazito ndipo alipohisi kusikia dirisha la chumba chake likigongwa. Wazazi wa Masumbuko walijenga nyumba ndogo, ya vyumba viwili vya kulala na sebule moja. Ilikuwa ni nyumba hafifu, iliyodhihirisha ufukara uliowatofautisha na familia za 'wenye nazo' mathalani akina Mzee Mkombo.



    Masumbuko alilala katika chumba kimojawapo. Chumbani mwake humo hakukuwa na chochote cha ziada, zaidi ya kitanda na ndoo moja ya plastiki aliyoitumia kuweka kibatari juu yake. Humo ndimo chumbani mwake, na alilala peke yake.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Kwa mara ya kwanza aliposikia dirisha likigongwa hakuyaamini masikio yake. Mara ya pili ndipo alipoamini akisikiacho. Akajitoa kitandani taratibu na kulisogelea dirisha hilo kwa kunyata.



    Alipolifikia, alitulia. Mara likagongwa tena. Akilini mwake aliamini kuwa mgongaji hakuwa na nia mbaya. Aligonga taratibu, ikiwa ni dhahiri kuwa hakutaka mtu mwingine asikie, mtu mwingine zaidi ya Masumbuko.



    Ni nani huyu? Masumbuko alijiuliza.





    Tena ni usiku! Mazingira ya nje yalikuwa tulivu sana, hali iliyotoa taswira kuwa watu wengi wamashalala majumbani mwao. Masumbuko hakuwa na saa wala redio ambayo labda ingemsaidia kubaini kuwa ni saa ngapi.



    Lakini hakupenda kujidanganya kuwa huenda ni saa 2 au saa 3. Hapana. Alikumbiuka kuwa yeye na wazazi wake walimaliza kula saa 4 kasoro dakika kadhaa wakati redio ya baba yake ilipokuwa ikitangaza.



    Baada ya mlo, baba na mama yake waliingia chumbani mwao na yeye akaingia chumbani mwake. Ni muda mrefu alikuwa akigaagaa huku masikio yake yakidaka sauti za wapita njia huko nje na ngurumo za magari zikiitawala anga kila baada ya dakika chache.



    Hatimaye kelele zile zilikoma. Ukapita tena muda mrefu. Kwa makisio ya karibu, alihisi kuwa muda huo alipokuwa akisikia dirisha likigongwa ni saa 5 au zaidi ya hapo.

    Wasiwasi huo ulidumu kwa dakika chache tu na kutokomea. Akapiga moyo konde, na kwa sauti ya chini akauliza, “Nani?”



    “Masumbuko, nifungulie.”



    Ilikuwa ni sauti laini ya kike, lakini haikuwa sauti ngeni masikioni mwa Masumbuko. Hivyo akapapasa kitandani na kukipata kibiriti ambacho alikitumia kuwashia kibatari. Kisha akafungua mlango wa chumbani mwake na kuufuata ule mlango mkubwa kwa mwendo uleule wa kunyata.



    Alipoufungua akakumbana na Happy. Ndiyo, alikuwa ni Happy yuleyule, Happy binti wa Mzee Mkombo, usiku huu akiwa amejitanda kanga kama mwari.



    Wakaongozana, Masumbuko mbele, Happy nyuma hadi chumbani mwa Masumbuko. Moja kwa moja Happy akafikia kitandani. Haijulikani alijisikia vipi pindi alipoketi kitandani hapo na kuuhisi ugumu wa ngozi ile ya ng'ombe. Kwao alikuwa akilalia kitanda bora cha thamani kubwa, chenye godoro nene, ndani ya chumba maridadi kilichosakafiwa saruji iliyomeremeta.



    Chumba cha kitajiri!



    Sasa yumo ndani ya chumba hiki dhaifu, ameketi katika kidubwasha ambacho Masumbuko hukiita kitanda. Ndani ya chumba chenye ukuta usiopigwa lipu; chumba kidogo chenye sakafu ya udongo, chumba ambacho paa lake ni nyasi zilizofungwa juu ya mianzi.



    Chumba cha kimaskini!



    Haijulikani alijisikia vipi moyoni japo usoni hakuonyesha kushangazwa na chochote wala kukerwa na lolote. Alionyesha kuridhika na mazingira aliyomo.





    Masumbuko alimfuata na kuketi kando yake. Akamtazama kwa mshangao. Kisha, kwa mnong'ono akamuuliza, “Imekuwaje, Happy?”



    Happy hakujibu. Aliinamisha uso, akauma midomo na kufinyafinya vidole vya mikono. Masumbuko aliendelea kumwangalia, na ndipo kumbukumbu ya yale yaliyojiri wakati wakichunga mbuzi zilipomjia kichwani. Hivyo akajua ni nini alipaswa kukifanya.



    Akaupeleka mkono kifuani pa Happy na kuifungua kanga ile. Akavishuhudia vititi vichanga na vyekundu mithili ya nyanya mbivu pale kifuani. Alipoitoa kanga ya pili, macho yakatua katika 'Bustani ya Edeni.'

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Happy akaingiwa na soni. Akajiinamia na kujikunyata pale kitandani. Alikuwa akihema kwa taabu. Labda alikuwa akihofu. Lakini alihofu nini? Kwani kafukuzwa huko kwao?



    Masumbuko akachukua hatua ya pili. Akakizima kile kibatari, kisha, safari ya mikono yake iliyotetemeka ikaanzia mgongoni mwa Happy, ikahamia katika zile 'nyanya' kifuani na kuishia pale mapaja yake yalipounganika.



    Kwa mbali akamsikia Happy akishusha pumzi ndefu na kuanguka kitandani. Kilichofuata ni kile ambacho Happy alikihitaji japo alikipokea kwa woga na kilikuwa ni kile ambacho Masumbuko alikipenda. Wakawa wamefungua ukurasa mpya katika uhusiano wao.



    **********



    HAPPY aliondoka saa 11 alfajiri. Aliondoka huku akiwa ameingia katika dunia mpya; ile himaya yake ya usichana ikiwa imeshavunjwa. Masumbuko, kwa upande wake aliona fahari. Aliwahi kusikia baadhi ya vijana wakijivunia kufanya tendo la ndoa na wasichana bikra, na wakawa ndio 'wafunguzi' wa himaya. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwake, na alijivuna kwa hilo.



    Tangu siku hiyo urafiki wao ukawa ni urafiki wa kikubwa; ukaimarika na kukomaa. Wakawa wakikutana mara kwa mara na kuuhudumia ujana wao.



    Hatimaye uvumi ukaanza kusambaa; kwamba Mzee Mkombo anakwenda California, Marekani kuongeza ujuzi wa kazi yake kwa teknolojia ya kisasa zaidi. Huko angelazimika kuishi miaka mitano. Lakini Masumbuko alipomdokeza Happy kuhusu uvumi huo, Happy alikanusha.



    “Hakuna kitu kama hicho, Masu.”



    “Lakini mbona uvumi huo umezagaa?” Masumbuko alimbana. “Tena inasemekana ataondoka na familia yake yote! Yaani utaniacha, Happy!”

    Happy alisonya. Kisha akasema, “Usisikilize maneno ya mitaani, Masu. Unisikilize mimi. Na kama itatokea hivyo n'takutaarifu haraka. Ya nini kukuficha? Tulia mpenzi.”



    Siku zilikuja, siku zikaenda. Hatimaye usiku mmoja, kitu kama saa 6 hivi, Happy alimgongea dirisha Masumbuko, na alipofunguliwa, jambo la kwanza alilofanya ni kumwambia: “Ni kweli, Masumbuko. Tunaondoka.”



    “Nini?”



    “Tunaondoka,” Happy alisisitiza. “Tunaondoka wote.”



    Ukimya ukatawala. Masumbuko na Happy wakabaki wakitazamana. Uso wa Happy ulijaa majonzi na wa Masumbuko ukiwa unashangaa.

    Kisha Happy akaendelea: “Sikiliza, mpenzi. Ni wewe ndiye mwanamume wangu wa kwanza, na ndiye utakayenioa. Nakuahidi kukutunzia mwili wangu huu. Sitambeba mwanamume mwingine yeyote kifuani pangu.”



    Akanyamaza na kumtazama Masumbuko kwa yale macho yake yenye simanzi. Moyo wa Masumbuko ukakaribia kupasuka kwa uchungu.

    Kisha, kwa msisitizo uleule, Happy akaendelea, “Lakini sitaki uendelee kuzubaa hapa Nzega, Masu. Kwa nini uendeleee kulemaa hapa ilhali umeshamaliza shule? Maisha yako hayatainuka, Masu. Huwezi kupata maendeleo kama utategemea kilimo na biashara ndogondogo zisizo na kichwa wala miguu. Habari nd’o hiyo!



    “Hivyo, nakuomba sana, tena sana, uondoke hapa Nzega. Ondoka, uende popote ukatafute maisha. Siyo kweli kuwa kila mwenye elimu kubwa ndiye anayeneemeka kimaisha. Hapana, hiyo ni imani potofu. Ondoka, ondoka mpenzi, Masu. Kasake maisha. Mimi nikirudi tu, tutafunga ndoa. Na itakuwa ni ndoa ya aina yake. Umenielewa mpenzi?”



    “Nimekuelewa, na nitajitahidi,” Masumbuko alilazimisha kuipata sauti yake. Kwa jumla hakuitarajia taarifa hiyo. Ilikuwa ni taarifa mbaya masikioni na moyoni mwake.



    Hata hivyo, kwa kuzingatia kuwa siku mbili zijazo zingewakuta Happy na wazazi wake angani wakielekea Marekani, wapenzi hao waliamua kuutumia usiku huo kama usiku maalumu kwa kuagana kwa maneno na vitendo.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Hatimaye siku ya tatu Happy aliondoka. Sasa maisha ya Masumbuko yakakosa msisimko. Vijana wenzake wakaaanza kumcheka na kumdhihaki. Na kwa ujumla mambo yalianza kumwendea kombo. Zawadi ndogondogo mathalani nguo, sukari na pesa alizokuwa akipewa na Happy sasa zilitoweka.



    Japo dakika ya mwisho kabla ya Happy hajakiacha kitanda cha Masumbuko usiku ule alimpatia shilingi 50,000 za 'kwa heri' hata hivyo hizo hazikuwa pesa za kumsukumia maisha kwa muda mrefu. Zilikatika wiki moja baadaye.



    Ndipo makali ya maisha yalipoanza kujidhihirisha kwa Masumbuko. Mji wa Nzega ukawa mchungu kwake. Na kadri siku zilivyokwenda ndivyo pia mambo yalivyozidi kumwendea vibaya.



    Akazikumbuka nasaha za Happy.



    **********



    WIKI mbili baada ya Happy kuondoka, Masumbuko alikata shauri. Ndiyo, aliamua kuufuata ushauri wa Happy. Akawaaga wazazi wake akiwaambia kuwa anataka kwenda mjini Tabora kutafuta kazi.



    “Mjini?” mama yake alimshangaa. “Huko mjini utafikia kwa nani, mwanangu?”



    “Kwa Zakayo,” Masumbuko alilaghai.



    “Zakayo?”



    “Ndiyo.”



    “Huyo Zakayo nd'o nani?”



    “Ni rafiki yangu wa siku nyingi,” Masumbuko aliukazia uongo wake. “Tulisoma pamoja. Kwa sasa anaishi huko mjini, kitongoji cha Isevya kwa baba'ake mdogo.”



    Mama yake aliguna. Akaendeleza udadisi. “Kwani hapa Nzega umeona huwezi kupata kazi?”



    “Kwa hapa Nzega ni vigumu sana, mama,” Masumbuko alikazi uasemi wake. “Ningeweza hata kwenda machimboni, lakini mambo ya madini yanahitaji ushirikina mwingi. Na mimi sitaki kujiingiza kwenye ushirikina.”



    Wazazi walikosa nguvu ya kuupinga uamuzi wa Masumbuko.



    Siku iliyofuata Masumbuko alikuwa ndani ya basi akielekea mjini Tabora. Mfukoni alikuwa na shilingi 70,000 tu na hakuwa na pa kufikia. Alimwomba Mungu kimoyomoyo amsaidie katika azma yake ya kujikwamua kimaisha kama alivyotakiwa na mpenzi wake, Happy.



    Basi liliingia mjini Tabora mchana. Alipoteremka, kitu cha kwanza alichokifanya ni kutafuta mgahawa ili ajipatie mlo wa gharama nafuu. Na alipoupata alikula huku akiwaza jinsi atakavyoyakabili maisha katika mji huo.



    Kwa kiasi fulani alihisi woga ukimnyemelea. Hata hivyo akapiga konde moyo na kuamua kutoka nje ya mgahawa, akienda kutafuta gesti. Hakufika mbali, mara akakutana na kijana mmoja aliyeitwa Solomon.



    Solomon alisoma shule moja na Masumbuko lakini Solomon alikuwa alikuwa mbele ya Masumbuko kwa madarasa mawili. Walipokutana hapo mjini Tabora, ni Masumbuko aliyeanza kumkumbuka Solomon. Akamsalimia na kujitambulisha kwa kirefu.



    Solomon akaisikiliza hadithi ya Masumbuko kwa kirefu kiasi cha kuingiwa na huruma.



    “Pole, sana,” Solomon alimwambia. “Mimi nahangaika tu hapa town. Nabeba mizigo pale sokoni.”



    “Soko gani?”



    “Soko kuu.”



    “Duh, si ni kazi ngumu sana?” Masumbuko alimuuliza kwa mshangao.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    “Hakuna kazi rahisi duniani mdogo wangu,” Solomon alimwambia. “Hata mimi siyo kwamba naifanya kazi hiyo kwa kuipenda. Hapana. Ni shida tu. Hata hivyo natarajia kuzamia Dar baada ya siku chache.”



    Waliongea kwa kirefu, na hatimaye Masumbuko akaamua kujiunga na Solomon katika kazi ya kubeba mizigo katika soko kuu la mjini Tabora.



    Miezi miwili baadaye, Masumbuko, Solomon na wenzao wawili wakaamua kulivaa jiji la Dar es Salaam kwa minajili ya kutafuta maendeleo zaidi.



    Waliipanda treni pamoja lakini Solomon na wale vijana wengine wawili waliteremkia Morogoro kinyemela bila ya kumtaarifu Masumbuko. Treni ilipoingia jijini Dar Es Salaam saa 6 mchana ndipo Masumbuko alipobaini kuwa wenzake walimtoroka.



    Sasa akajikuta akikabiliana na mazingira magumu zaidi. Hii ilikuwa ni mara yake ya kwanza kuingia jijini Dar. Afanye nini?

    “Mimi ni mwanamume,” alijiambia na kujipa ujasiri. Akawa tayari kukabiliana na hali yoyote itakayojitokeza.



    Kwa siku tatu mfululizo akawa akila mihogo ya kukaanga mitaani na wakati mwingine akijipatia mlo kwa akinamama lishe; wali, maharage na kushushia maji mengi katika kuongeza ujazo tumboni. Usiku ulipoingia alijichimbia katika majengo ambayo ujenzi wake haujakamilika na kutoka alfajiri ya siku inayofuata.



    Hatimaye akaamua kuirudia ile kazi yake aliyoiacha kule Tabora. Katika siku hizo tatu alikuwa akishinda kwenye vijiwe vya kahawa na ni hapo aliposikia simulizi nyingi kuhusu jiji hilo. Na ndipo pia aliposikia kuwa kuna soko kubwa katika eneo la Kariakoo, soko ambalo vijana wengi huenda kufanya kazi za kubeba mizigo hapo.



    Kwa kuwa aliishi katika jiji geni, na alihitaji kupata pesa ya kula na matumizi mengine, ikibidi hata kupata nauli ya kumrudisha Nzega, aliamua kulisaka hilo soko la Kariakoo.



    Siku chache baadaye alikuwa akifanya vibarua vya kubeba mizigo kutwa nzima katika soko hilo.



    Masumbuko akawa hapati hata muda wa kuoga wala kufua nguo. Akawa mchafu kupindukia. Sasa hakutofautiana na taahira. Lakini hakuacha kujishughulishsa na kazi hiyo ya kubeba mizigo . Aache, halafu ale nini?



    Wiki moja baada ya kuanza kazi hiyo, siku moja kitu kama saa 5 hivi, alimwona mama mmoja mnene aliyekuwa na mizigo iliyomwelemea.



    Alikuwa bado yu mwanamke mbichi japo unene ulimvamia kwa nguvu. Kwa mtazamo wa harakaharaka alimwona mwanamke huyo kama awezaye kumkomboa na dhiki iliyomzunguka.



    Akamsogelea kwa mwendo wa taratibu. Kisha “shikamoo” ikamtoka.

    Mwanamke yule aligeuka na kumtazama. Akajiwa na huruma pale macho yao yalipokutana. Aliibaini dhiki iliyogubika katika maisha ya Masumbuko kupitia katika macho yake. Naam, macho ya Masumbuko hayakuhitaji maelezo ya ziada katika kumtambulisha kuwa yuko katika lindi la matatizo.



    “Marahaba, hujambo?”



    “Sijambo, mama yangu,” Masumbuko alijibu. Kisha, papohapo akaongeza, “Samahani, mama, naomba nikusaidie mizigo yako. Mimi siyo kibaka. Nina kama wiki moja na nusu tangu niingie hapa mjini. Kwetu ni Nzega. Kwa kweli nina maisha ya taabu sana tangu nifike hapa.”



    Mama yule alitua mizigo chini kisha akamkazia zaidi macho Masumbuko. Akatikisa kichwa kwa huruma.



    Alimwona kuwa ni kijana ambaye amejaaliwa sura nzuri na umbo zuri, lakini furaha ambayo ilitakiwa kujidhihirisha katika uso wake ilifichwa katika macho yale yenye kila aina ya majonzi na dhiki ya maisha. Hiyo ilikuwa bayana kufuatia ngozi yake iliyokauka, nywele chafu na timtim sanjari na mavazi chakavu yaliyomsitiri maungoni.



    Nyuma ya huruma iliyomwingia mwanamke huyo, kulikuwa na kitu kingine kilichopenya katika mtima wake, kitu ambacho hakielezeki kwa ufasaha, lakini kilichomfanya achukue uamuzi wa kumsaidia Masumbuko mara moja.



    Akamwambia, “Beba mfuko huo twende kwenye gari lilee...” alimwonyesha kwa kidole.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    Masumbuko alifanya kama alivyoelekezwa. Akavibeba vifurushi vile na kuviingiza katika buti la gari, Mercedes Benz jeusi. Kisha akaambiwa aingie garini. Takriban saa nzima baadaye walikuwa Bunju 'A', nje ya jumba kubwa la kifahari.



    Eneo hilo la Bunju 'A' halikuwa na nyumba nyingi, lakini hizo chache zilizokuwapo hazikuwa za kawaida. Baadhi zilikuwa ndogo na baadhi zilikuwa kubwa, lakini zote zilivutia.



    Kwa vyovyote vile, kwa Mtanzania wa kawaida, ambaye huishi kwa kupata mlo mmoja kwa siku, akiziona nyumba hizo hataamini kuwa ni za Watanzania wenzake, na kama ataambiwa kuwa ni za Watanzania basi haitamwingia akilini kuwa pato walilotumia kwa kuzijenga nyumba hizo ni la halali.



    Miongoni mwa nyumba hizo ni jumba hili ambalo gari hili limeegeshwa nje yake, na Masumbuko kukaribishwa ndani.



    Naam, kwa mara ya kwanza Masumbuko akajikuta ndani ya sebule ambayo hajapata kuiona tangu azaliwe. Masofa makubwa yenye umbo la kobe, meza na viti vinavyoendeshwa kwa mitambo maalumu, televisheni kubwa iliyojengewa eneo maalum ukutani, na zulia lipumualo ni baadhi tu ya samani zilizomshangaza.



    “Karibu, karibu ujisikie kama uko kwenu...umesema kwenu ni wapi vile?” mama yule alimtazama usoni huku akiachia tabasamu la mbali.



    “Nzega.”



    “Yeah, Nzega. Basi ujione kama uko Nzega, Unyamwezini.”



    “Asante, mama,” Masumbuko aliitika huku bado kasimama. Alionekana bado akiendelea kuustaajabia umaridadi wa sebule ile.



    “Keti tu hapo sofani,” yule mama alimwambia. “ Mbona unasitasita? Keti wala usihofu.”



    Masumbuko aliketi. Yule mama naye akaketi katika sofa jingine.



    “Mimi naitwa Chausiku. Na...” akasita kidogo kisha akaita kwa sauti kali, “Mwanahawa!”



    “Bee!”



    “Njoo!”



    Muda mfupi baadaye binti mmoja akaingia, akamtupia macho kidogo Masumbuko kisha akayahamishia kwa Chausiku.



    “Na huyu ni Mwanahawa,” Chausiku aliendelea huku akimtazama Masumbuko. “Anaitwa Mwanahawa. Ni mdogo wangu, baba mmoja, mama mmoja.”



    Masumbuko aliitika kwa kutikisa kichwa huku akimtazama Mwanahawa. Huyu Mwanahawa alifanana sana na Chausiku. Lakini kufanana huko kulikuwa ni kwa sura tu, kwa maumbile walitofautiana sana.



    Chausiku alikuwa ni mnene, tipwatipwa wakati Mwanahawa alikuwa na mwili mdogo lakini katanuka mapajani na kulitengeneza umbo la 'nane.' Akilini mwa Masumbuko, Mwanahawa alivutia zaidi na hata angestahili kushiriki kwenye kinyang'anyiro chochote cha ulimbwende.



    Hata hivyo hakupata muda wa kumtazama zaidi Mwanahawa, mara Chausiku akamuuliza, “Na wewe jina lako ni nani?”



    “Masumbuko.”



    “Masumbuko?” Chausiku alimuuliza, akionekana kutomwamini.



    “Ndiyo, Masumbuko.”

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

    *****MASUMBUKO KALIVAA JIJI LA DAR NA KUKUMBANA NA SHIDA KIBAO, LAKINI SIKU MOJA KAPATA MKOMBOZI. NI MKOMBOZI KWELI AU MKOMBOZI BANDIA?



    ITAENDELEA



0 comments:

Post a Comment

Blog