Search This Blog

Monday, October 24, 2022

FACEBOOK CHATTING - 3

 





    Chombezo : Facebook Chatting

    Sehemu Ya Tatu (3)




    Ilipoishia 


    nikaamka na kisha kuangalia kioo cha simu ile, namba haikuwa imehifadhiwa simuni lakini kwa kuiangalia tu, nilikuwa nikiijua, ilikuwa ni namba ya Juliet. Huku nikionekana kuwa katika uchofu, nikabonyeza kitufe cha kijani na kisha kuipeleka sikioni.




    Songa nayo sasa....


    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/


    JULIET: Mambo Nyemo!
    MIMI: Poa. Mzima wewe?
    JULIET: Mimi mzima. Upo wapi?
    MIMI: Nyumbani.
    JULIET: Njoo basi hapa uwanja wa ndege. Nimekwishafika, nataka unipeleke hotelini.
    MIMI: (Kitu cha kwanza, usingizi wote pamoja na uchovu nilio nao vikatoweka, Juliet alikuwa amefika mkoani Kagera kwa ajili ya kuja kuonana nami, nilishtuka, nikaanza kujihukumu kwa kujiona kwamba nilikuwa nimemdanganya kwamba naishi Kagera kumbe ukweli ni kwamba nilikuwa naishi Dar es Salaam alipokuwa akiishi. Katika kipindi hicho, sikujua nimjibu nini zaidi ya kukaa kimya huku mwili nikiuhisi umepigwa na ganzi)


    JULIET: Haloooow......!


    Bado nilionekana kuchanganyikiwa kupita kawaida, kitendo cha Juliet kufika ndani ya mkoa wa Kagera ndicho kilikuwa kitu ambacho kilinichanganya sana. Nilibaki kimya huku nikikipa kichwa changu nafasi zaidi ya kufikiria juu ya kile ambacho nilitakiwa kumwambia kwa wakati huo. Juliet aliendelea kuita zaidi na zaidi huku nami nikijifanya kama kutokusikia, tayari nilikuwa sipo sawa kichwani.


    JULIET: Mbona haunijibu chochote Nyemo?
    MIMI: Ninaogopa kukukasirisha.
    JULIET: Kivipi?
    MIMI: Nilikudanganya.
    JULIET: Ulinidanganya? Kunidanganya nini?
    MIMI: Kwamba nilikuwa nikiishi Kagera, ila ukweli ni kwamba siishi huko.
    JULIET: Thats too bad Nyemo. Kwa nini umenidanganya hivi mpaka kuharibu fedha na kuja huku? Kwa nini umenidanganya Nyemo?
    MIMI: Samahani.
    JULIET: Unafikiri itasaidia chochote kile Nyemo?
    MIMI: Hapana. Ila naomba unisamehe.
    JULIET: Nikusamehe kwa hili ulilonifanyia Nyemo? Kupoteza zaidi ya laki sita na nusu kwa hili ulilonifanyia Nyemo?
    MIMI: (Kimyaa)
    JULIET: Sawa mkali wangu, nimekuelewa. Naomba uniambie ukweli sasa. Upo wapi?
    MIMI: Nipo Dar es Salaam.
    JULIET: Unaishi wapi?
    MIMI: Naishi Tandale.
    JULIET: Nitapanda ndege leo jioni kuja huko, nitataka kuonana na wewe.
    MIMI: Sawa (Simu ikakatwa)


    Kwanza nikashusha pumzi ndefu na kisha kuanza kujutia kile ambacho nilikuwa nimekifanya. Nilijua dhahiri kwamba Juliet alikuwa akinipenda sana lakini sikuwa na jinsi, kwa wakati huo moyo wangu ulikuwa kwenye majonzi mazito na nilidhani labda katika kipindi ambacho ningemuona Juliet katika macho yangu na kisha kumuomba msamaha face to face ndicho kingekuwa kitu ambacho kingenifanya kuwa na amani moyoni mwangu.
    Saa kumi na moja jioni, simu yangu ikaanza kuita, nilipoangalia namba, ilikuwa ni ya Juliet. Mapigo yangu ya moyo yakaanza kudunda kwa kasi, nilikuwa na maswali mengi kichwani mwangu juu ya Juliet huyu, nikapiga moyo konde na kisha kuipokea.


    MIMI: Hallooow
    JULIET: Hallow.
    MIMI: U mzima?
    JULIET: Mzima tu. Upo wapi?
    MIMI; Nipo nyumbani. Umeshafika Dar?
    JULIET: Tayari nimekwishafika. Nataka kuja kwenu sasa hivi. Nitafikaje hapo?
    MIMI: Upo wapi?
    JULIET: Nyumbani.
    MIMI: Wapi?
    JULIET: Osterbay.
    MIMI: Sawa. Cha msingi nenda kituoni na kisha upande daladala inayokwenda Ubungo kutoka Msasani au Masaki.
    JULIET: Hapana Nyemo. Nakuja na gari langu binafsi.
    MIMI: Okey! Kama ni hivyo njoo hapa Morocco ya Magomeni, si unapajua?
    JULIET: Ndio.
    MIMI: Ukifika hapo si kuna barabara inaelekea Sinza?
    JULIET: Ndio.
    MIMI: Njoo na hiyo barabara.
    JULIET: Sawa. Nipe dakika ishirini (Simu ikakatwa)
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Nikabaki nikiwa na presha kubwa. Katika presha ambayo nilikuwa nayo kwa wakati huo ni sawa na shabiki wa mpira wa miguu ambaye alikuwa akienda kuiangalia timu yake inayotarajia kucheza na timu ambayo ina uwezo mkubwa zaidi ya timu yake. Nilibaki nikiwa sijui nifanye nini. Kitu cha kwanza ambacho nilikuwa nimekifikiria ni kuanza kufanya usafi wa kizushi chumbani kwangu. 


    Kwa wavulana watakuwa wanaelewa uharaka ambao anakuwa nao mvulana wa kufanya usafi mara msichana anaposema nipo njiani nakuja kwenu. Kila shuka ambalo nilikuwa nikilitandika kitandani nilikuwa naliona chafu, yaani hata shuka ambalo nilikuwa nimelifua jana yake nalo lilikuwa likionekana chafu. 


    Nilichokifanya ni kuchukua shuka jingine ambalo kwa kidogo sana lilikuwa likipendeza machoni mwangu na kisha kulitandika. Nikafagia chumba haraka haraka, nikafuta vumbi, nikachukua air freshner na kisha kuipulizia chumba kizima na kufunga pazia ili kuifanya harufu ile isitokea nje na kuisha. Nilipoona kila kitu kipo poa, kandambili zangu za kuendea chooni na bafuni nikazitupia uvunguni pamoja na ufagio wangu wa chelewa. 


    Baada ya kila kitu, nikaanza kukiangalia chumba kile, bado sikuridhika kabisa. Nikaelekea chumbani kwa kaka yangu na kisha kuchukua mito na kuipeleka kitandani kwangu, viatu ambavyo vilikuwa vimekaa ovyo ovyo nikavitupia chini ya uvungu wa kitanda.


    Kwa maandalizi ambayo nilikuwa nimeyafanya, Juliet kwangu akaonekana kama malkia ambaye alikuwa akija kunitembelea siku hiyo. Nilipoona kila kitu kimekaa sawa, nikatulia nikiwa nimekaa sakafuni kwani kama ningekaa kitandani, ningeweza kulivuruga shuka lile na kujikunja jikunja. Wala hazikupita dakika nyingi, simu yangu ikaanza kuita, nilichokifanya ni kuipokea.


    JULIET: Nimefika hapa wanapaita Kwa Tumbo.
    MIMI: Okey, Pandisha hicho kilima cha juu mpaka huku mwisho.


    Bado nilikuwa nikiendelea kumpa maelekezo Juliet mpaka pale ambapo macho yangu yakaanza kuiona gari aina ya X Trail fulani ya Bluu ambayo ilikuwa ikija kwa mwendo wa taratibu. Kwa sababu alikuwa amekwishaniambia kwamba angekuwa ndani ya gari hilo, nilipoona limekaribia, nikalisimamisha kwa kupunga mkono na kisha Juliet kufungua kioo cha mlango wa mbele.


    Naomba nieleweke jamani....kwa hapa ningependa nieleweke na watu wote mnielewe kwa umakini kabisa. Yaani....yaani....yaani.....Mmmh! Kiukweli ni kwamba kwa miaka ishirini na tatu na nusu ambayo nimeishi katika dunia hii nimekutana na wasichana wengi warembo ila kwa huyu Juliet ambaye nilikuwa nikimwangalia, alionekana kuwa zaidi.


    Juliet alikuwa mrembo, tena mrembo zaidi ya warembo ambao niliwahi kukutana nao katika maisha yangu yote. Nilibaki nikimwangalia Juliet, Mungu wangu! Alikuwa mrembo hasa tena zaidi ya mrembo. Kama watu wanavyosema kwamba Malkia wa Misri, Cleopatra alikuwa mrembo zaidi ya wanawake wote wa duniani mpaka sasa, ila nafikiri mtu ambaye aliyesema hayo hakuwa amemuona Juliet, msichana huyu alikuwa mrembo sana kiasi ambacho sikuwa nikiishiwa kumsifia.


    JULIET: Vipi! Mbona unanishangaa hivyo?
    MIMI: Wewe ndiye Juliet?
    JULIET: Ndiye mimi.
    MIMI: Ndiye ambaye ulikuwa umesafiri kuelekea Kagera kunifuata?
    JULIET: Ndiye mimi.
    MIMI: Hapana. Wewe ndiye ambaye nilikuwa nimekuficha kwamba sikai Dar es Salaam?
    JULIET: Ndiye mimi.
    MIMI: Kweli wakati mwingine unaweza kujiona una akili kumbe ni mburula kabisa.
    JULIET: Kivipi?
    MIMI: Mimi ni Mburula...tena kiongozi wa mamburula wote duniani. Haiwezekani nikudanganye mtu kama wewe.
    JULIET: Kwa nini?
    MIMI: Dah! Twende nyumbani kwanza.


    Juliet akateremka kutoka garini. Kwanza watu wote ambao walikuwa pembeni na mahali pale wakaonekana kushangaa kupita kawaida, uzuri wa Juliet haukuonekana kuwa wa kawaida hata mara moja. Najua kwamba Mungu alikuwa akiwaumba duniani katika matumbo ya mama zao lakini kwa Juliet akili yangu ilikuwa ikikataa kabisa kwamba hakuwa ameumbwa tumboni mwa mama yake bali alikuwa ameshushwa moja kwa moja kutoka huko kwa Mungu na kuletwa duniani kwa lengo moja tu, kunijaribu mimi tu.


    Vipi kuhusu umbo, utazumzungumzia vipi Juliet. Alikuwa mrembo sana tofauti na picha za uongo ambazo alikuwa ameziweka facebook. Tulitembea huku tukipiga stori, akili yangu kwa wakati huo ilikuwa ikikifikiria chumba changu tu, sikujiamini kama chumba kile nilikuwa nimekiacha katika hali ya usafi. Tulitembea huku tukipiga stori huku yeye akiwa amebeba begi dogo mgongoni, tulipofika nyumbani, tukaingia chumbani.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Tulipofika chumbani, nikapigwa na mshangao mkubwa sana, na si mimi peke yangu ambaye nilitakiwa kupigwa na mshangao huo bali hata kama ungekuwa wewe ni lazima ungepigwa na mshangao pia. Chumba nilikiacha katika mazingira ya usafi wa hali ya juu ambao sikuwahi kuufanya ila nilipoingia sasa hivi pamoja na Juliet, chumba kilikuwa shaghalabaghala. 


    Shuka lilikuwa lipo ovyo ovyo, viatu na kandambili ambavyo nilikuwa nimeviweka uvunguni vilikuwa vimetolewa, harufu ya air freshner ambayo nilikuwa nimeipulizia wala haikuwa ikisikika, vumbi lilikuwa likionekana, mito ambayo niliichukua kwa broo wala haikuonekana kitandani, yaani kama chumba kilivyokuwa kabla ya kufanya usafi ndivyo kilivyokuwa kwa wakati huu, mbaya zaidi, hata sufuria niliyopikia ugali ambayo niliitoa nje na kuiweka kwenye karo, eti nayo ilikuwa chumbani huku maji na mwiko vikiwa ndani ya sufuria hiyo niliyoiloweka ili ukoko uliokuwa umeganda utoke.


    JULIET: Chumba kizuri.




    Mwili wangu ulikuwa umenyong’onyea kupita kawaida, nilikuwa nikikiangalia chumba kile huku nikionekana kupigwa na mshangao mkubwa kupita kawaida. Macho yangu sikutaka kuyapeleka usoni mwa Juliet kwani nilikuwa najisikia noma kupita kawaida. Muda wote Juliet alikuwa akikiangalia chumba kile huku akitabasamu kupita kawaida, hali ambayo aliikuta chumbani mle dizaini ikaonekana kumfurahisha.


    MIMI: Dah!
    JULIET: Kuna nini tena.
    MIMI: Kuna jamaa nilimwachia chumba toka juzi mimi nilikwenda kulala msibani, kanipa funguo kumbe hata chumba hajakifanyia usafi. Siku nikimnyima ataanza kulalamika (Nilidanganya)
    JULIET: Sasa kwa nini ulimpa ufunguo mtu ambaye unajua si msafi?
    MIMI: Huwa ninampa kila siku hasa ninapoona kwamba silali chumbani. Sasa sijui kwa nini kafanya hivi. (Niliongea kimajonzi kana kwamba ilikuwa kweli)
    JULIET: Pole sana.
    MIMI: Usijali. Ngoja nikisafishe.


    Hapo hapo nikaanza kukisafisha chumba hicho huku kichwa changu kikiendelea kufikiria juu ya namna ambavyo chumba kile kilivyokuwa kimechafuliwa namna ile. Kiukweli ni kwamba nilichanganyikiwa, kitu ambacho kilitokea kilionekana kunichanganya kupita kawaida. Juliet hakutaka kuniachia mimi tu nifanye usafi wa chumba kile, nae akaanza kunisaidia.


    Tulianza kwa kufanya usafi wa chumba kile na kisha kuosha vyombo. Nilishangaa sana kwani kwa akili yangu nilikuwa nikiwaza kwamba Juliet alikuwa mtoto wa ushuwani, msichana ambaye toka alipozaliwa alimkuta mfanyakazi wa ndani ambaye alikuwa akifanya kazi zote, kwa hiyo niliamini kwamba asingeweza kufanya usafi kama kuosha vyombo.


    Mawazo yangu na kile nilichokiona vilikuwa vitu viwili tofauti, Juliet alikuwa akiosha vyombo vizuri kabisa kiasi ambacho mpaka nilishangaa. Tuliendelea na usafi mpaka pale ambapo tulimaliza na ndipo tukakaa chini na kupumzika huku chumba kikionekana kung’aa zaidi ya mara ya kwanza.


    MIMI: Asante kwa msaada wako.
    JULIET: Usijali. Karibu.
    MIMI: Poa.
    JULIET: Kuna kitu naomba nikugawie kama zawadi.
    MIMI: Kitu gani na zawadi ya kwa ajili ya nini?
    JULIET: Huwa unaandika hadithi na kutuwekea facebook kwa kutumia kompyuta ipi?
    MIMI: Ile pale.
    JULIET: Huwa unapenda kuitumia hiyo?
    MIMI: Si sana kwani ina uwezo mdogo.


    Hapo hapo Juliet akalifungua begi ambalo alikuja nalo na kisha kutoa kompyuta moja ya mapajani (laptop) na kisha kunigawia. Kwanza sikuamini kama kompyuta ile nilikuwa napewa mimi, nikaifungua na kisha kuangalia ni ya aina gani, ilikuwa ni APPLE ya kisasa, toleo jipya kabisa ambayo dukani katika kipindi hicho ilikuwa si chini ya milioni mbili na nusu.


    JULIET: Zawadi yako hii kama shukrani zangu kwa kunifurahisha na hadithi zako facebook.
    MIMI: Asante sana (Nilijibu huku macho yangu yakiendelea kuiangalia laptop ile)
    JULIET: Kuna kingine unachokihitaji?
    MIMI: Hapana. Nafikiri hapa umenisaidia vya kutosha ila nina wasiwasi.
    JULIET: Wasiwasi wa nini?
    MIMI: Na hawa matanesco. Kwa tabia zao za kukata umeme na kurudisha mara kwa mara wanaweza kuiunguza hata hii laptop yenyewe.
    JULIET: Usijali. Hii ina chombo chake maalumu cha kupoza umeme ambacho kimewekwa humo humo ndani.

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    MIMI: Asante sana Juliet. Hapa umenisaidia sana. Sijui niseme nini kuonyesha shukrani kwako.
    JULIET: Usijali. Yote ninafanya haya kama shukrani.


    Siku hiyo tuliongea mengi kama marafiki wa kawaida, akili yangu ilikuwa tofauti na jinsi nilivyokuwa nikifikiria kabla kwa kuona kwamba Juliet angeniambia maneno mengi kuhusiana na mapenzi, alikuwa tofauti kabisa. Hakuonekana kutaka kuongea kuhusiana na mahusiano hata kidogo, alikuwa akiongea kirafiki sana kiasi ambacho nilizidi kushangaa zaidi na zaidi moyoni mwangu. Mpaka katika kipindi ambacho anaondoka chumbani pale, nilikuwa siamini kama kweli aliweza kuondoka huku akiwa hajazungumza kitu chochote kile kuhusiana na mapenzi.


    Urafiki wangu na Juliet ukazidi kuongezeka zaidi na zaidi lakini haukunifanya niache kuchati na kipenzi changu, barafu wa moyo wangu, Dorcas ambaye katika kipindi hicho alionekana kuchanganyikiwa kwenye mapenzi yangu. Maisha yangu kwa wakati huo yalikuwa ya raha kupita kawaida, kulia nilikuwa na rafiki ambaye alikuwa akinijali sana, Juliet huku kushoto nikiwa na mpenzi ambaye alikuwa akinipenda na kunithamini sana, Dorcas.


    Nikajiona mimi ndio mimi, nilikuwa nikihitaji nini tena cha zaidi katika maisha yangu? Hakukuwa na cha zaidi. Ukaribu wangu na Juliet ulizidi kuongezeka zaidi na zaidi mpaka kufika kipindi ambacho nikaanza kwenda kwao, akanitambulisha kwa wazazi wake kwamba mimi nilikuwa rafiki bora katika maisha yake. Juliet hakuishia hapo, akawaambia kwamba nilikuwa nikiandika hadithi katika mtandao wa facebook kitu ambacho kiliwashtua sana. Baba yake, mzee Lyimo akaanza kuniangalia kwa mshangao.




    MZEE LYIMO: Unaandika hadithi? (Aliuliza huku akionekana kushtuka)
    MIMI: Ndio mzee.
    MZEE LYIMO: Huwa unaandika hadithi za namna gani?
    MIMI: Za kusisimua na hizi za riwaya (Sikutaka kuzitaja za chombezo, si unajua ningeweza kuharibu kila kitu)
    MZEE LYIMO: Safi sana. Nataka kukupa kazi moja.
    MIMI: Kazi gani?
    MZEE LYIMO: Kwanza huwa ukiandika hadithi unategemea kupata kiasi gani?
    MIMI: Huwa siandiki kwenye magazeti. Ila kwenye magazeti unaweza kupata hata milioni tatu mpaka hadithi yako inakwisha.
    MZEE LYIMO: Na kama umeandika kitabu?
    MIMI: Bado sijajua. Ila kama una wateja wengi zaidi ya elfu kumi, basi unaweza kupata hata milioni sabini.
    MZEE LYIMO: Safi sana Nyemo. Nahitaji unifanyie kitu fulani halafu nitakulipa hiyo milioni sabini. Au hata milioni mia moja kama utakubali kunifanyia kazi hiyo.
    MIMI: (Huku nikionekana kushtuka) Kazi gani?
    MZEE LYIMO: Nitataka uniandikie kitabu cha maisha yangu yaliyopita mpaka sasa hivi, utatakiwa kuunganisha stori ya mke wangu Susan pamoja na yangu. Nitakuhadithia, kazi yako itakuwa ni kuandika tu.
    MIMI: Sawa. Nitafanya hivyo.
    MZEE LYIMO: Ila hizo milioni mia moja zitakutosha au nikuongeze?
    MIMI: Zitanitosha sana.
    MZEE LYIMO: Sema bwana usije ukatangaza kuwa nimekunyonya.
    MIMI: Zitanitosha sana.


    Unajua wakati mwingine nilikuwa nikijiona kama naota ndoto moja nzuri na ya kufurahisha sana kiasi ambacho sikutaka kuamka, ila ukweli ni kwamba hapo sikuwa naota bali kilikuwa ni kitu halisi ambacho kilikuwa kikitokea katika maisha yangu. Baba yake Juliet, mzee Lyimo alikuwa akitaka niandike stori ya maisha yake pamoja na mkewe, niziunganishe na hatimae kiwe kitu kimoja. Hilo lilionekana kuwa dili kubwa ambalo sikutarajia kulipata katika maisha yangu. 


    Sikukaa sana nyumbani hapo, mara baada ya kuongea vya kutosha, nikaaga na kisha kuondoka nyumbani hapo huku Juliet akinisindikiza na gari lake. Hakutaka nielekee moja kwa moja nyumbani, tukapitia kwenye mashine ya ATM, akatoa kiasi cha shilingi milioni moja na nusu na kisha kunigawia shilingi milioni moja, nilishangaa sana.


    MIMI: Juliet.....!
    JULIET: Usishtuke. Twende kwenye ule mghahawa tukale kwanza.


    Tukaanza kuelekea kwenye mghahawa ule na kisha kutakiwa kuagiza chakula. Nikapewa menu na kuanza kuiangalia. Kulikuwa na aina ya vyakula zaidi ya sabini ila vyakula ambavyo nilikuwa nikivijua ni viwili tu, rice na chips, vingine sikuwa nikivijua kabisa.


    JULIET: Unataka nini?
    MIMI: Mix Grill (Nilimwambia Juliet huku hata chakula hicho sikukijua kinafafanaje).
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Mhudumu akaitwa na kisha kuambiwa kuleta vyakula ambavyo tulikuwa tumeagiza. Ndani ya dakika kumi, vyakula vilikuwa mezani, tukala na kisha kuanza kuangaliana huku kila mmoja akionekana kuwa na shauku ya kutaka kumwambia mwenzake jambo fulani.


    JULIET: Unajua kwamba baba naye ana akaunti facebook?
    MIMI: Hapana.
    JULIET: Anayo. Nilimfungulia mwaka jana, ila hatumii jina lake.
    MIMI: Kwa nini sasa?
    JULIET: Hataki tu. Ila pamoja na hayo, yeye ndiye aliyenifanya nipende kusoma stori zako.
    MIMI: Kivipi?
    JULIET: Mara nyingi baba alikuwa yupo bize sana na mtandao wa facebook kiasi ambacho hadi mama alikuwa akikasirika sana. Kila alipokuwa akimuuliza kwa sababu gani, alikuwa akijibu kwamba hadithi zako ndizo ambazo zilikuwa zinamfanya kuwa bize. Basi na mimi nikamuomba aniambie kuhusu page yako, akaniambia kwamba ni NYEMO THE PRINCE, nika-like na kisha kuanza kupata burudani. Huwezi amini Nyemo, kwa sasa wewe ni rafiki wa familia nzima, ila pale baba hakutaka kujionyesha kwamba naye ni mmoja wa fans wako.
    MIMI: Dah!
    JULIET: Ndio hivyo, hadi mama naye akafungua akaunti ya facebook na kisha kuanza kusoma stori zako. Unaposema kwamba itaendelea, tunakuwa na mzuka wa kutaka kujua itaendelea vipi. Unapokaa kimya na kutokutoa kwa siku, tunaonekana kama kuumwa siku hiyo.
    MIMI: Poleni sana.
    JULIET: Asante. Baba anakukubali sana na ndio maana ameamua kutaka kukupa shavu hili la kumwandikia kitabu cha maisha yake.
    MIMI: Asijali. Nitaifanya kazi hiyo.
    JULIET: Unakumbuka kuna kipindi ulilalamika kuhusu tatizo la kompyuta yako kuungua chaja?
    MIMI: Nakumbuka.
    JULIET: Basi hali hiyo ikamfanya kukununulia laptop nchini Marekani kwani alikuwa huko kipindi hicho. Alipokuja, akanipa na kutaka nikuletee ila nisikwambie kwamba ni yeye ndiye aliyenipa nikupe.
    MIMI: Hahaha! Sasa kwa nini umeniambia?
    JULIET: Basi tu. Hata hizi fedha aliniambia nikupe zikusaidie kwa kuweka vifurushi ili usiache kutoa hadithi hata siku moja.
    MIMI: Duuh!
    JULIET: Ndio hivyo.


    Kwa wakati huo nikajiona kupata zali kubwa sana ambalo wala sikuwa nimelitegemea katika maisha yangu, kukutana na familia ambayo ilikuwa na utajiri mkubwa ilinifanya kujiona kwamba na mimi nilikuwa nakwenda kuwa tajiri muda wowote ule. Juliet hakutaka kunificha, alikuwa akinielezea kila kitu ambacho sikuwa nikikifahamu. Hapo ndipo nilipojua kwamba baba yake, mzee Lyimo alikuwa tajiri mkubwa na mfanyabiashara ambaye alikuwa akijulikana sana. Alikuwa na biashara nyingi kubwa ambazo kwa siku zilikuwa zikimuingizia zaidi ya milioni themanini kwa mwezi.


    Kwangu hata kabla sijakiandika kitabu cha maisha yake nikajiona kuridhika, fedha hazikuwa mikononi mwangu lakini tayari nilikuwa nimekwishazipangia bajeti na kilikuwa kimebakia kiasi cha shilingi milioni arobaini tu, milioni sitini zilikuwa zimekwishakwisha. Maisha yaliendelea zaidi mpaka siku ile ambayo mzee Lyimo akaniita na kisha kukaa katika maktaba ndogo ambayo ilikuwepo ndani ya nyumba yake na kisha kuanza kunielezea historia ya maisha yake.


    Usikivu wangu ulikuwa mkubwa sana, nilikuwa nikimsikiliza kwa makini kabisa. Historia ya maisha yake ilikuwa ni ya kusikitisha iliyojaa umasikini mkubwa kiasi ambacho wakati mwingine niliona kama alikuwa akinidanganya. Kila alipokuwa akielezea, muda mwingi nilikuwa nikishusha pumzi nzito na kisha kumsikiliza zaidi. Alitumia muda wa masaa mawili, historia ikawa imekamilika na hivyo kumuita mke wake ambaye nae akaanza kunielezea yake.


    Najua kuna watu ambao walikuwa wamepitia katika umasikini ila kwa watu hawa wawili nadhani walikuwa wamezidi zaidi ya watu wote. Historia zao kwa pamoja kwangu mimi zilionekana kuwa kama filamu fulani ya Kitanzania ambayo iliandikwa na mwandishi mahili kwa sasa nchini Tanzania, mwandishi ambaye anaonekana kuibadilisha jamii, Andrew Carlos


    Mara baada ya kusikiliza historia zao kwa pamoja, hapo ndipo nilipotakiwa kuanza kazi yangu. Nikaitoa laptop kutoka katika begi ambalo nilikuja nalo na kisha kumtaka mzee Lyimo achukue muda wa dakika ishirini kuniambia historia ya maisha yake, akaanza kunihadithia, alipomaliza, nikavipeleka vidole vyangu katika keyboard ya kompyuta ile, nilipoyainua macho yangu, nilikuwa nimeandika zaidi ya kurasa thelathini na kisha kumuonyeshea kwanza aisome kabla hatujaendelea.


    MZEE LYIMO: Kweli wewe mtu umezaliwa kwa ajili ya kuandika tu, umeandika vizuri zaidi ya nilivyokuwa nikifikiria.
    MIMI: Usijali mzee. Kazi yangu mimi ni kuandika tu, sina kazi nyingine niliyopewa, sina kipaji kingine maishani mwangu. Uandishi ndio kazi yangu na ndio kipaji changu.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Mzee Lyimo akaendelea zaidi na zaidi kunihadithia huku nami nikiandika kama kawaida yangu. Siku hiyo nilitumia masaa manne kuandika historia ya maisha yake na ndipo nikaondoka huku hata nusu ikiwa haijafika. Katika wiki nzima nilikuwa nikiifanya kazi yake hiyo, kuandika historia ya maisha ya mtu haikuwa kazi ndogo, ilikuwa ni aina ya hadithi ya kweli ambayo iliwahi kutokea, hivyo haukutakiwa kuongeza neno lolote wala kupunguza kutoka kwake.






    Mzee Lyimo alikuwa akitambua utu, kila nilipokuwa nikienda kwake na kurudi nyumbani, alikuwa akinikabidhi kiasi cha shilingi elfu hamsini kama pole ya kazi kubwa ambayo nilikuwa nikiifanya siku hiyo. Uandishi wa simulizi ya maisha yake nilitumia siku sitini na ndipo ikakamilika huku katika siku zote akiwa amenigawia elfu hamsini kama pole, kwa hiyo ndani ya miezi miwili nilikuwa nimekwishachukua milioni tatu nje ya malipo yangu ya milioni mia moja,
    Baada ya historia yake kuisha, hapo ndipo nikaanza na historia ya mke wake, Bi Susan ambaye naye alikuwa na historia ambayo ilikuwa ikinishangaza sana. Kama kawaida, malipo ya siku yalikuwa yale yale huku nikila pale pale nyumbani kwao. Kwa Bi Susan wala sikuchukua muda mrefu, ndani ya mwezi mmoja na nusu nikawa nimekwishamaliza kuandika historia yake na kisha kuwagawia na kuanza kuzisoma. Uandishi wangu uliwafurahisha sana.


    Baada ya siku mbili, nikazionganisha historia zile pamoja na kitabu kukamilika na kisha kwenda kukichapisha huku jina la kitabu hicho likiitwa MY WIFE AND I. Nilimuuliza juu ya jina la kitabu kuwa la Kingereza ila aliniambia kwamba alipenda iwe hivyo kwani alikuwa akitaka kukiuza kitabu hicho katika nchi mbalimbali kwa ajili ya wale watu ambao walikuwa wamekata tamaa ya maisha waweze kufarijika na kujiona kwamba walikuwa na nafasi ya kufanya mambo fulani katika maisha yao.


    MZEE LYIMO: Kitabu hiki kitauzwa dunia nzima, ningependa niongee na maisha ya watu kupitia maisha yetu yaliyopita. Kitatafsiriwa kwa lugha nne, Kiswahili, Kifaransa, Kingereza na Kihispania
    MIMI: Hapo itakuwa vizuri sana. Kupitia maisha yenu kumeonekana kunibadilisha hata mimi.
    MZEE LYIMO: Umejifunza nini kupitia maisha yetu?
    MIMI: Nimejifunza kwamba hakuna kukata tamaa katika maisha na pia hatutakiwi kuuogopa umasikini zaidi ya kupambana nao kama ambavyo mlivyofanya.
    MZEE LYIMO: Kuna kingine ulichojifunza?
    MIMI: Labda niseme kwamba mnapokuwa watu wawili, upambanaji wenu hauwi mgumu sana kama ambavyo utakuwa peke yako.
    MZEE LYIMO: Na hiyo ndio pointi yenyewe. Bila mke wangu, nadhani nisingeweza kufika hapa nilipokuwa kwa sasa, yeye ameonekana kuwa msingi mkubwa wa maisha yangu, yeye ameonekana kuwa mafanikio yangu makubwa sana katika maisha yangu. Amekuwa mwanamke mwerevu sana, naweza kusema ni mwerevu zaidi ya wanawake wote katika dunia hii.
    MIMI: Ningetamani kuwa na mke mwenye hali ya kujituma kama mke wako, mwanamke ambaye atakuwa akinifariji na kunitia nguvu katika maisha yangu bila kujali ni maisha gani ya shida tunayopitia.
    MZEE LYIMO: Juliet yupo, amechukua tabia kama za mama yake, ana damu ya mama yake, japo si mkubwa sana lakini tayari nimeona kuna mengi amerithi kwa mama yake.
    MIMI: Anaonekana kuwa msichana mwerevu sana ambaye anajali na kusikiliza. Nimeufurahia urafiki wangu pamoja nae.
    MZEE LYIMO: Unakiona kitabu hiki ulichokiandika?
    MIMI: Ndio.
    MZEE LYIMO: Mpaka sasa hivi watu walioweka oda ni watu elfu sitini duniani na bado wengine wanazidi kumiminika kwa wastani wa watu elfu kumi kwa wiki. Nitakwenda kuingiza fedha nyingi sana, zaidi ya bilioni tano duniani.
    MIMI: Duh! Kumbe uliangalia mbali.
    MZEE LYIMO: Sana. Nitaingiza zaidi ya bilioni tano, halafu wewe nikulipe milioni mia moja, hauoni kwamba huo ni unyonyaji?
    MIMI: Ila nimeridhika na malipo yangu.
    MZEE LYIMO: Hapana Nyemo. Ni lazima nifanye kitu fulani kwa ajili yako, ninataka kubadilisha maisha yako kabisa, yaani yabadilike kwa asilimia mia moja. Kwa kutumia fedha hizo, nitakujengea nyumba ya thamani na kukununulia gari la thamani sana pamoja na kukufungulia biashara kubwa ambazo zitakuwa zako, una kingine unachokihitaji?
    MIMI: Hapana. Nafikiri vinatosha na nitashukuru sana.
    MZEE LYIMO: Okey! Au unamtaka nikuongezee na binti yangu?
    MIMI: Hapana. Bado mapema mno.
    MZEE LYIMO: Sawa. Usijali. Nashukuru sana. Nadhani ungeniachia namba ya akaunti yako ya benki ili nikuingizie fedha hizo. 


    Hapo nikamuandikia namba ya akaunti yangu na kisha kuondoka mahali hapo. Ndani ya gari nilikuwa nikionekana kuwa mwingi wa furaha kwani kwa wakati huo nilijiona kuwa tajiri mkubwa sana japokuwa kiasi ambacho nilitakiwa kukipata ni milioni mia moja tu. Kwa jinsi ambavyo furaha ilivyokuwa moyoni mwangu, nilitamani nipae angani na kisha kuitangazia dunia kwamba nilikuwa nimeingiza kiasi cha shilingi milioni mia moja kwa wakati huo.
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Nilipofika nyumbani pamoja na Juliet, tukateremka kutoka garini na kisha kuanza kuelekea kilipokuwa chumba changu. Njiani nikakutana na rafiki yangu, Thomas Lyaruu ambaye akanifuata huku uso wake ukionekana kuwa na majonzi.


    MIMI: Vipi tena?
    THOMAS: Kuna taarifa mbaya.
    MIMI: Kuhusu nini?
    THOMAS: Kumbe Dorcas alifariki.
    MIMI: Alifariki? Lini?
    THOMAS: Toka mwaka jana alipokuwa shuleni nchini Uganda.
    MIMI: Dorcas alifariki toka mwaka jana alipokuwa nchini Uganda! Kivipi tena? Mbona hata juzi nilikuwa nae?
    THOMAS: Acha utani. Ulikuwa naye juzi juzi?
    MIMI: Tena hata namba yake ya simu ninayo hapa.
    THOMAS: Hebu mpigie.


    Nikachukua simu yangu kutoka mfukoni na kisha kuanza kuitafuta namba ya Dorcas ambaye nilikuwa katika mahusiano pamoja naye. Katika kipindi hicho nilionekana kushtuka sana, ilikuwaje Dorcas awe amefariki toka mwaka jana na wakati nilikuwa nikiwasiliana naye huku mara nyingi akija nyumbani pale. Kwa kiasi fulani nilikuwa nimechanganyikiwa. Juliet alibaki kimya huku akiniangalia, niliangalia namba ile katika simu yangu, sikuiona japokuwa nilikuwa nimeisave.


    THOMAS: Ipo wapi?
    MIMI: Eti siioni na wakati niliisave.
    THOMAS: Hebu acha utani Nyemo, iweje namba uisave halafu usiione?
    MIMI: Hata mimi nashangaa.
    THOMAS: Kwa hiyo unasema kwamba ulikuwa ukionana na Dorcas?
    MIMI: Ndio. Tena hata juzi alikuja hapa nyumbani.
    THOMAS: Alikuja muda gani? Mbona sikumuona?
    MIMI: Huwa anakuja usiku.
    THOMAS: Mimi ni rafiki yako wa karibu, sasa kwa nini hukuniambia nije nionane naye?
    MIMI: Nilitaka kufanya hivyo ila alikuwa akikataa kabisa.
    THOMAS: Kwa nini alikuwa akikataa?
    MIMI: Sijui.
    THOMAS: Alipokuwa akiondoka ulikuwa ukimsindikiza?
    MIMI: Hapana.
    THOMAS: Kwa nini?
    MIMI: Alikuwa akikataa pia.
    THOMAS: Kuna kitu.
    MIMI: Kitu gani?
    THOMAS: Umekwishawahi kukisoma kitabu cha A Beautiful Girl from Hell kilichoandikwa na Padwer Simpson?
    MIMI: Hapana.
    THOMAS: Huyo hakuwa Dorcas.
    MIMI: Hakuwa Dorcas? Sasa alikuwa nani?
    THOMAS: Alikuwa jini.
    MIMI: Whaaaaaaat?


    Dizaini kama sikuwa nimemuelewa Thomas Lyaruu ila kwa wakati huo ilinipasa nimuamini. Huyu ni rafiki yangu mkubwa, ni rafiki yangu mkubwa kuliko marafiki wote duniani kwa sasa, hakuwahi kunitania katika jambo kama hili japokuwa mara nyingi sana huwa tunafanya utani katika mambo mengine. Nilimwangalia Thomas huku macho yangu yakionekana dhahiri kutokuamini kile ambacho nilikuwa nikikisikia masikioni mwangu. Nikayageuza macho yangu na kumwangalia Juliet.


    Macho ya Juliet yalikuwa yakionyesha hofu kubwa, alionekana kuogopa kile ambacho alikuwa amekisikia kwa wakati huo. Hapo ndipo picha fulani ikaanza kunijia kichwani mwangu. Kwa kukukumbusha nafikiri unajua kwamba Dorcas alikuwa mpenzi wangu, alikuwa akinipenda kama ambavyo nilikuwa nampenda katika kipindi hicho. Kwa sababu alikuwa mpenzi wangu, hivyo alikuwa akisikia wivu kama ambavyo nilikuwa nikisikia wivu katika moyo wangu.


    Ninachokihisi katika kipindi ambacho nilikuwa nawasiliana na Juliet alikuwa akihisi wivu sana na ndio maana hata katika kile kipindi ambacho nilikuwa nimesafisha chumba changu na kisha kwenda kumpokea Juliet, nilikikuta chumba kikiwa shaghalabaghala. Jibu juu ya kile kitu ndicho ambacho kilinijia kichwani mwangu kwa wakati huo.


    MIMI: Jini!
    THOMAS: Ndio maana yake.
    MIMI: Inawezekana vipi lakini?
    THOMAS: Ngoja nikuulize swali Nyemo.
    MIMI: Uliza.
    THOMAS : Unasema kwamba Dorcas alikuwa mpenzi wako, si ndio?
    MIMI: Ndio.
    THOMAS: Na ulisema alikwishawahi kuja chumbani kwako mara nyingi, si ndio hivyo?
    MIMI: Ndiyo.
    THOMAS: Mlikwishawahi kufanya mapenzi?
    MIMI: Hapana. Alikuwa akikataa katakata.
    THOMAS: Hukuwahi kuota ndoto za kufanya naye mapenzi?
    MIMI: Niliwahi. Nilikuwa naota sana ndoto za namna hiyo. Nilikuwa nikifanya naye mapenzi sana ndotoni.
    THOMAS: Hivyo ndivyo majini yalivyo, mara nyingi huwezi kufanya nao mapenzi hivi hivi, hukufuata ndotoni kama ambavyo Padwer Simpson alivyoeleza katika kitabu chake cha Beautiful Girl From hell.
    MIMI: Sawa. Nimekubali, ila nataka kuamini zaidi.
    THOMAS: Unataka kuamini nini tena?
    MIMI: Ngoja niende nyumbani kwao.
    THOMAS: Sio uende, twende wote, si unapajua?
    MIMI: Ndiyo. Nilikwishawahi kufika.
    THOMAS: Uliwahi kuingia ndani ya nyumba yao?

    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    MIMI: Hapana. Alinionyeshea tu na kisha kuondoka.
    THOMAS: Basi sawa. Twende.
    JULIET: Na mimi nataka kwenda. Ni wapi?
    MIMI: Magomeni.


    Hatukutaka kuchelewa mahali hapo, tulichokifanya ni kuanza kulifuata gari la Juliet na kisha kuondoka mahali hapo. Nilionekana kuwa kama mtu ambaye nilichanganyikiwa kwa wakati huo, maneno ya Thomas ambayo aliniambia kwamba Dorcas alikuwa jini yalionekana kunichanganya kupita kawaida.


    Kutoka nyumbani Tandale mpaka magomeni wala hapakuwa mbali sana hivyo kwa kutumia gari tulitumia muda wa dakika tano tukawa tumekwishafika na kisha kuelekea mapipa ambapo alikuwa akiishi Dorcas. Njia nilikuwa nikizikumbuka sana, nilikuwa nikielekeza mpaka pale ambapo nilijua fika kwamba ndipo alipokuwa amenionyeshea kwamba ndio palikuwa kwao.


    MIMI: Mhhh!
    THOMAS: Vipi tena?
    MIMI: Mbona kuna mbuyu?
    THOMAS: Wapi?
    MIMI: Hapa ndipo kulipokuwa nyumba yao, nashangaa kuna mbuyu.
    THOMAS: Unamaanisha kwamba hapa ndipo alipokuonyeshea kwamba kuna nyumba yao?
    MIMI: Ndio hapa. Nashangaa kuna mbuyu.
    THOMAS: Una uhakika kwamba ni hapa?
    MIMI: Ndio. Ni hapa tena hadi ndani niliingia kila nilipokuja kumtembelea.
    THOMAS: nadhani unanitania Nyemo.
    MIMI: Kweli tena Thomas. Siwezi kukutania katika hili.


    Wakati mwingine nilikuwa naongea kama utani lakini ndivyo nilikuwa nikimaanisha, nilionekana kushangaza kupita kawaida, sehemu ambayo Dorcas alikuwa amenionyesha kwamba kulikuwa na nyumba yao kwa wakati huo kulikuwa na mbuyu mmoja mkubwa ambao ulikuwa ukisifika sana Magomeni kwa mambo ya kishirikina kutoka na kila siku watu kuujaribu kuukata mbuyu huo lakini haukuwa ukikatika kabisa.


    Nilipojaribu kumtafuta Dorcas hata katika mtandao wa marafiki zangu Facebook, sikuweza kumuona, sikuweza kuziona tena meseji zake ambazo alikuwa akinitumia, jina la akaunti yake likapotea kabisa katika mtandao wa facebook. Masikini Dorcas, msichana ambaye nilikuwa nikimpenda ndio alikuwa amekufa nchini Uganda toka mwaka jana katika mapigano ya kisiasa nchini humo katika kipindi cha uchaguzi alipokuwa chuoni. Kuanzia siku hiyo, sikuweza kumuona tena Dorcas mpaka katika kipindi hiki, hakurudi tena katika maisha yangu hadi pale nilipomuoa Juliet, hakuwa amerudi. 


    Kwa sasa, nimefanikiwa katika maisha yangu, Juliet ndiye msichana ambaye nimemuoa na hatimae kunipatia mtoto mdogo wa kume aitwaye Henry mwenye miaka 4. Hiyo ilikuwa historia fupi ambayo nimejaribu kukupa katika kipindi ambacho nilianzisha uhusiano na msichana jini ambaye nilikuwa nimezoeana nae na nilikuwa nikimpenda sana katika kipindi cha nyuma.


    Umasikini ambao nilikuwa nao, nilikwishauaga na kwa sasa nipo huku katika visiwa vya Hawaii nchini Marekani kwa ajili ya kula maisha na mke wangu mpendwa Juliet pamoja na mtoto wetu, Henry. Kuandika hadithi kwangu facebook ndio kulinipa utajiri nilionao kwa sasa hasa mara baada ya kukutana na baba mkwe, mzee Lyimo ambaye alibadilisha sana maisha yangu.


    Napenda sana kuyazungumzia maisha yangu ya nyuma katika kipindi ambacho nilikuwa masikini wa kutupwa. Leo hii ukisema ni kitu gani ambacho ninakichukia katika maisha yangu, nitakwambia umasikini. Najua wapo wengi ambao wanaandika hadithi facebook ila ningependa kuwaambia kitu kimoja tu, usimdharau mtu yeyote katika mtandao huu kwani mtu huyo anaweza kubadilisha maisha yako katika staili ambayo wala hautoweza kutegemea.


    Kwa sababu sikuwa nikimdharau mtu, hata nilipoonyeshewa jina analolitumia mzee Lyimo, nilishangaa sana. Alikuwa akitumia picha ya mtu mwingine, alikuwa akipenda sana kuLIKE na kuCOMMENT post zangu pamoja na hadithi mbalimbali. Alikuwa akinirekebisha sana na kunikosoa pale nilipokuwa nafanya makosa, kuna watu kiukweli walikuwa wakimdharau bila kumjua ila kwangu alikuwa mmoja wa watu muhimu sana. Mara nyingi nilikuwa nikijiuliza kwamba kama ningeweza kumdharau leo ningekuwa wapi? Natumaini nisingekuwa katika visiwa hivi, nafikiri nisigeweza kupata milioni mia moja, nyumba ya kifahari, magari ya kifahari pamoja na miladi mingi.


    Kwa kumalizia tu, bado naendelea kusisitiza kwamba si kila msichana au mvulana unayemuona ndani ya mtandao wa facebook ni binadamu, kuna wengine huwa majini, majini ambayo yamekuwa yakihangaika huku na kule kutafuta damu za watu. Kwa Dorcas, alikuja kwangu kama mwili wake na nilikuwa nikimfahamu, ila kiukweli kama nisingekuwa namfahamu, tayari angekuwa amekwishanimaliza. 
    CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
    Kwa kumalizia naomba ujue kwamba hii ni hadithi ya kutunga tu ambayo nilipewa wazo na huyu rafiki yangu Thomas Lyaruu Jnr. Aliponipa wazo la kuandika kijistori hiki kifupi, nilikipuuzia kwa muda wa mwezi mzima, ila nilipokiandika, kiukweli kimeonekana kueleweka sana.


    MWISHO WA SEASON 2, ENDELEA NA SEASON 3


    ITAENDELEA

0 comments:

Post a Comment

Blog